Tumeona katika utangulizi wa makala hii ndefu ya kwamba wakati mipango ya Serikali ya Uingereza kwa ajili ya hali ya baadaye ya Serikali Palestina iliposhindwa kufua dafu dhidi ya kampeni ya Wazayoni ya Mabavu, mnamo 1947 iliamua kulikabidhi suala hili Umoja wa Mataifa. Suala la hali ya baadaye ya Serikali ya Palestina lilitawala mjadala katika Baraza kuu la usalama la Umoja wa Mataifa.

General Assembly iliteua Kamati Maalum iliyojulikana kama (UNCSCOP) — yaani United Nations’ Special Commission for Palestine, kushughulikia suala hili. Septemba 3, 1947, Kamati ilisikilisha kwa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mipango miwili:- Majority Plan (yaani mpango wa walio wengi) na Minority Plan (yaani mpango wa wachache).

Mpango wa wengi ulipendekeza usitishwaji wa Mamlaka na ugawanywaji wa Palestina, uundwaji wa Dola ya Waarabu na ile ya Wayahudi zenye mwelekeo wa kiuchumi kati yao na Corpus Separation kwa ajili ya Mji wa Jerusalem ambao (ungekasimiwa) na utawala maalumu wa kimataifa na kuongozwa na Umoja wa Mataifa.

Mpango wa walio wachache —ulipendekeza pia kusitishwa kwa Mamlaka, lakini ukapendekeza uanzishwaji wa Dola ya Shirikisho (Federal State) ambayo ingejumuisha Dola ya Wayahudi na ile ya Waarabu Jerusalemu yakiwa makao makuu.

Katika mjadala uliofuatia, Waarabu waliugomea mpango kwa msingi kuwa ulikuwa ukivunja haki zao na ulikuwa ukikinzana na sheria na kanuni kuu za demokrasia. Zaidi ya hapo walihoji, mamlaka, nguvu ya umoja wa mataifa kugawanywa kwa ardhi yao katika dola mbili na hivyo kuvuruga hadhi yao ya kimipaka (territorial integrity).

Wazayuni waliunganisha nguvu zao kupata uungwaji mkono wa kura ya Umoja wa Mataifa kwa ajili ya ugawaji wa Palestina. Yakiwa ni matokeo ya shinikizo za kisiasa (zitakazoelezwa baadaye) Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa Novemba 29, 1947 liliridhia kwa kura 33 kwa 13. Kura 10 zilikuwa nje ye mahudhurio. Hii ilimaanisha Azimio la kugawanywa kwa Palestina, kwa mantiki ya mpango wa walio wengi (Majority Plan) ilikubalika.

Kuridhiwa kwa Azimio la kugawanywa kwa Palestina kulizua wimbi la malalamiko, maandamano na usumbufu usio kifani ndani ya Palestina. Waarabu walikuwa wamedhamiria kupinga kugawanywa kwa nchi yao. Kwa upande mwingine Wayahudi walikuwa wamejipanga kuunda Dola ya Wayahudi ndani ya Palestina.

Kamisheni ya Palestina iliyoteuliwa na Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa kutekeleza mpango wa ugawanywaji (Partition) wa Palestina haikutimiza wajibu wake. Umoja wa Mataifa haukuwa na nguvu ya kuzuia mlipuko wa mgogoro ambao umekuwa ukirindima tangu kuridhiwa kwa Azimio April 16, 1948. Kikao Maalum kilifanyika kwa lengo la kutafakari kwa kina hali ya baadaye ya Serikali ya Palestina.

Hata hivyo, kikao kilimalizika Mei 14, 1948 kwa kuteua Msuluhishi, bila uamuzi wowote kufanyika juu yahali ya baadaye ya Palestina. Siku iliyofuata mamlaka iliishia katika dimbwi la vurugu na msigano usioelezeka. Je, unafahamu nini kiliendelea baada ya hapo? 

ITAENDELEA>>

 

Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa:-

(+255) 784 – 142 137 au (+255) 713 – 333 141

Barua pepe:

[email protected] / [email protected]

By Jamhuri