Na Bashir Yakub

Ushahidi wa kuambiwa ni ushahidi unaotolewa na mtu ambaye hakuona tukio likitendeka, hakusikia tukio likitendeka, hakuhisi wala kuonja, wala kunusa hilo, bali aliambiwa na mtu mwingine aliyeona, kusikia, kuhisi, kunusa au kuonja.  Zifuatazo ni sababu kwanini ushahidi huu haukubaliki:-

(A)  Sheria ya Ushahidi Kifungu cha 61 na 62 kinauweka ushahidi wa kuambiwa katika ushahidi wa maneno (oral evidence). Na kanuni za ushahidi wa maneno ni kuwa ili uweze kukubalika kama ushahidi sahihi ni lazima kama swali ni nani aliyeona tukio likitendeka, basi  jibu awe nalo mtu aliyeona tukio likitendeka, na kama swali ni nani aliyesikia tukio likitendeka, jibu awe nalo aliyesikia tukio likitendeka, na kama swali ni nani aliyehisi au kuonja kitu fulani, jibu awe nalo mwenyewe kabisa aliyehisi au kuonja kitu hicho, na kama swali ni mtaalamu yupi alipima na kugundua kuwa jambo fulani lilisababishwa na kadha wa kadha, jibu awe nalo mtaalamu huyohuyo na si vinginevyo. 

Hii ndiyo kanuni inayoongoza ushahidi wote wa maneno (oral evidence).  Kwa hiyo kwakuwa ushahidi wa kuambiwa nao ni ushahidi wa maneno lakini uliokosa sifa hii, basi mtu aliyesikia kutoka kwa mtu aliyeona ushahidi wake hauwezi kukubalika kwa kuwa atapingana na kanuni hii inayotaka mwenyewe kabisa aliyeona, kusikia au kuhisi kuwa ndiye awe shahidi. Hii ni sababu ya kwanza ya kutokubalika ushahidi wa kuambiwa au ushahidi wa nilimsikia akisema.

(B) Pili, ushahidi wa kuambiwa hautolewi kwa kiapo. Kawaida shahidi hutakiwa kuapa mahakamani kabla ya kutoa ushahidi na kiapo ndicho kitu pekee ambacho huthibitisha kuwa mtu anachosema ni kweli na kweli tupu. Ikiwa mtu atatoa ushahidi bila kuapa, ushahidi huo hauwezi kuitwa kweli na kweli tupu. Kwa mujibu wa sheria ya ushahidi, mtu anayetakiwa kuapa ni yule aliyeona tukio, kusikia, kuhisi, kuonja au kuthibitisha kitaaluma. Huyu ndiye anayetakiwa kuapa. Kwa maana hii aliyeambiwa anaweza kutoa ushahidi lakini bila kuapa kwa sababu hairuhusiwi kwake kuapa. Na kama haapi, ushahidi wake kuanzia hapo huwa sawa na bure, usio na maana yoyote, halikadhalika usiokubalika. 

(C) Pia haukubaliki kwa kuwa ni ushahidi ambao ni  mwepesi kuharibiwa. Hii ni kwa sababu aliyeona au kusikia ni tofauti na aliyeambiwa.  

Aliyeona au kusikia si rahisi kusahau alichokiona, au kukishika, lakini aliyeambiwa ni rahisi kusahau alichoambiwa chote au sehemu yake au nukta kadhaa za  alichoambiwa. 

 Hali hii ya kuwepo kwa uwezekano wa kusahau  huwa  inamtoa nje mtu huyu aliyeambiwa kwa kuwa muda wowote anaweza kuharibu ushahidi kwa kusahau nukta kadhaa kwa kuongeza au kupunguza, hivyo kuathiri uhalisia. Hii ni kawaida hata wewe ukitumwa ukampe maagizo mtu fulani hautatoa maagizo vilevile na kwa maneno yaleyale kama aliyekuagiza alivyosema. Utaongeza au utapunguza.

(D) Mwisho,  ushahidi wa kuambiwa haukubaliki kwa kuwa ni ushahidi unaoacha kiu. Ushahidi mzuri ni  ule unaomaliza kiu ya mahakama na ya kila mtu. Hii ni kwa sababu ushahidi wa kuambiwa  mpaka mtu aliyeambiwa anapomaliza kutoa ushahidi wake bado kila mtu katika mahakama hubaki akiwa na hamu ya kumuona au kumsikia aliyeona tukio kwa macho yake na akamsimulia huyu aliyetoa ushahidi. 

Kila mtu hubaki na swali la sijui huyu jamaa aliyeshuhudia yuko wapi. Hii ndiyo kiu inayobaki na kuufanya ushahidi huu kutojitosheleza. Ni sawa na wewe uambiwe na mtu aitwaye PATRICK kuwa alimsikia ALOYS akisema alimuona SAMUEL akichoma  moto nyumba yako.  Bila shaka utapenda zaidi kumuona  ALOYS  ili akwambie kilichotokea  kuliko PATRICK  anayekusimulia ambaye  hakuwapo.

By Jamhuri