Simba Watinga Bungeni, Wabunge Wawashangilia

Wachezaji na Viuonozi wa timu ya Simba sc
Wachezaji, Viongozi na baadhi ya Wabunge ambao ni wapenzi wa timu hiyo wakiwa kwenye picha ya pamoja

Timu ya Simba wametinga Bungeni jijini Dodoma leo baada ya kupata mwaliko wa Spika Job Ndugai.
Mwenyekiti wa Bunge, aliyekuwa akiongoza kikao cha leo, Najma Giga, Naibu Waziri wa Tamisemi, Joseph Kakunda ndiye alianzisha shangwe za kuwapokea Simba bungeni kabla hawajatambulishwa.
Kakunda kabla ya kujibu swali bungeni, alisema, leo ameamka saa 10 alfajiri akijiandaa kujibu maswali lakini furaha ya ubingwa wa Simba ilitawala kichwa chake hali ambayo ilipelekea wabunge wengine kushangilia.
“Sasa naamini Watanzania watapata wawakilishi wazuri wa michuano ya kimataifa, hawatatupa presha,” alisema Kakunda.
Mbunge wa Ilala, Dar es Salaam, Idd Azzan Zungu (CCM), alisema; “Humu ndani ya bunge kaingia mnyama mkali sana (Simba), lakini msihofu tuko salama,” wabunge wakaripuka shangwe tena.
Mbunge wa Mpwapwa (CCM), George Lubereje naye amewapongeza Simba akisema wamefanya kazi kubwa kuchukua ubingwa huo hata kabla ligi kumalizika.