Leo nina neno kwa wafanyakazi waliopo katika sekta mbalimbali za umma na za binafsi. Nimeamua kuandika waraka huu wa uchumi kwa wafanyakazi kutokana na sababu kuu tatu. Mosi, uwepo wa mbinyo wa kuongezeka kwa gharama za maisha ikilinganishwa na vipato halisi vya wafanyakazi.

Pili, kuwapo kwa uwezekano wa wafanyakazi kujikwamua kiuchumi kupitia ujasiriamali. Tatu, hata kama wafanyakazi wasipoona umuhimu wala ulazima wa kuongeza vipato vyao; bado ni kundi linaloweza kuliokoa taifa hili kwa kutengeneza maelfu ya ajira ikiwa wataamua kufanya hivyo.


Wafanyakazi wengi (japo yaweza kuwa si wote) watakubaliana na mimi kwamba mishahara na marupurupu yanayotolewa ajirani hayatoshelezi mahitaji ya kimaisha. Gharama za maisha zimepanda, mfumuko wa bei unazidi kutikisa nchi, na imefika mahali watu hawaelewi waishi vipi.

Upandaji wa maisha hauendani na ongezeko la mshahara, malengo ya kimaisha si tu kwamba hayatimii; lakini pia hayawezi kutimia kama mtu ataendelea kutegemea namna ile ile ya kipato – mshahara na marupurupu.


Yapo mambo mawili ningependa kila mfanyakazi afahamu. Cha kwanza ni kuwa; mabadiliko tunayoshuhudia nchini, yakiwamo ya kupanda kwa gharama za maisha na mfumuko wa bei ni ambayo yanaikumba dunia nzima, si Tanzania pekee.


Kwa maana hiyo, utatuzi wa suala hili ni kuachana na kufikiria kienyeji (local thinking) badala yake watu tufikirie kiupana (global thinking). Sambamba na hilo ni vema mtu mmoja mmoja kuwa na mtazamo chanya kuhusu ramani ya maisha kwa ujumla.


Cha pili ni kuwa; siasa haziwezi kuamua hatima yako isipokuwa umeziruhusu kufanya hivyo. Labda niiseme falsafa yangu kuhusu siasa ndipo naweza kueleweka zaidi; “Politics has nothing to do with my destiny”. Maana ya falsafa yangu hii ni kwamba siasa zinaweza kunizuia kwa muda kufika ninakotaka, lakini haziwezi kunizuia milele.


Nikisema hivi simaanishi ninaukana umuhimu wa siasa katika ustawi wa kiuchumi kwa wafanyakazi na mtu mmoja mmoja, isipokuwa ninachotaka turekebishe ni ile hali ya kudhani siasa zitafanya kila kitu maishani mwetu.


Nimeyataja mambo hayo mawili ili kusafisha njia ya kuelekea kwenye fikra pevu kuhusu uhuru wa kiuchumi kwa wafanyakazi. Kila mfanyakazi ni vema akafahamu kuwa usalama wa maisha yake hauwezi kuletwa na ongezeko la mshahara. Bila kulitambua na kulikubali hili tunaweza kuwa shidani; kwa sababu mara nyingi mtaji wa wanasiasa kupitia kura huwa ni ongezeko la mishahara!


Wanauchumi tunafahamu vizuri mchezo unaotokea wakati serikali inapoongeza mishahara pasipo kuongeza tija ya uzalishaji. Iko hivi, unapoongeza mzunguko wa fedha, (unbalanced injection of money into circulation) mfano kwa kuongeza mishahara kinyume na mizani ya kiuchumi; ikiwa hakuna tija katika uzalishaji basi unakuwa ukiibua mfumuko wa bei (inflation).


Mataifa madogo na makubwa hadi ninapoandika makala haya yanasumbuliwa na kusuasua kwa uchumi. Wanapojaribu kushusha ‘inflation’ wanajikuta wametengeneza uhaba mkubwa wa ajira, wanapojaribu kumimina ajira mitaani wanajikuta mfumuko wa bei unainua pembe zake.


Hata hivyo, nikiri kuwa inawezekana kuleta msawazo wa ujazo wa fedha na mfumuko wa bei; lakini kufanikiwa kwake kunategemea visababishi vingi mno (simulation factors) ambavyo kutokana na utamaduni wa nchi yetu kiuchumi; si rahisi kuvifanikisha vyote. Yote katika yote; hizo ni lugha na misamiati ya wachumi; lakini ni nini maana yake kwa mfanyakazi?


Hayo yanatupa kutambua kwamba kumbe usalama wa maisha ya mfanyakazi utapatikana kwa kujifunza mbinu za kuutumia mshahara kidogo anaoupata kuzalisha mifumo, bidhaa na huduma zitakazomwongezea tija. Hili linaweza kufanikishwa kwa mfanyakazi kuanzisha miradi midogo midogo nyumbani au mikubwa mahali pengine, kufungua biashara na hata kutumia vipawa alivyonavyo nje ya ajira yake kuzalisha fedha.


Nianze sasa na yale mambo matatu yaliyonisukuma kuwaandikia waraka huu, nikianza na lile la kwanza. Udogo wa mishahara isiyoendana na gharama za maisha unazidi kuleta msiba katika nchi yetu.


Hebu fikiria, mfanyakazi analipwa mshahara mdogo ambao akishalipa kodi ya nyumba, akanunua chakula, akafanya matumizi mengine ya msingi; kila mwisho wa mwezi anajikuta ana madeni. Tangu Januari hadi Desemba mfanyakazi huyu anakuwa ni mtu si tu wa madeni ila ni madeni yanayoongezeka. Hana tumaini la kujikwamua kesho wala keshokutwa.


Kutokana na hali hii tumezalisha wafanyakazi wengi ambao wajibu wao wameugeuza kama hisani kazini, ndiyo hawa ambao hawawezi kukuhudumia hadi umewapa chochote. Wengine wameendelea ‘ku-survive’ kwa kuungaunga, wanaishi kwa mizinga kila wakati na kila sehemu. Huwezi kuwalaumu; wanalazimishwa na mazingira yanayowakabili.


Nchi sasa hivi ina ‘mamilionea’ bandia ambao wamepata fedha zao kwa njia ya kughushi mikataba, kupewa hongo, kupokea rushwa kubwa na ndogo pamoja na wizi wanaoufanya kazini. Wakishapata fedha hizo ndipo wanajenga majengo makubwa makubwa, wananunua magari ya kifahari na kuishi maisha ya kifalme. Wengi wetu tumeingia katika mtego wa kuwasifu watu wa namna hii ya kwamba ni ‘wajanja’, ‘watafutaji’, ‘wenye akili’, ‘matajiri’ na majina mengine yenye sifa.


Kuna athari mbili kubwa mfanyakazi unaposhawishika kupata mafanikio kwa njia zisizo halali. Mosi ni kwamba unaliangamiza taifa na kuwadhulumu wengine. Pili, unaharibu utu wako wa ndani na kupoteza amani ya rohoni. Iko hivi; kikawaida uovu humrudia muovu, wema humrudia mwema.

Ukijikusanyia mali ama fedha kwa njia ya wizi, rushwa, hongo ama ujanja-ujanja; utajikuta unaishi maisha yasiyokuwa na amani hali inayosababisha kukosekana kwa furaha maishani mwako. Kikawaida mtu unapaswa uwe na mafanikio yanayoleta utulivu katika roho na nafsi yako; kinyume cha hapo haina maana ya kuwa na mafanikio.


Najua wapo watu mnaowafahamu ambao wametajirika kwa njia za mikato; nanyi mnaona kama wanaishi maisha mazuri yenye  furaha; ukweli wanaujua wenyewe kama ambavyo tunathibitishiwa na wataalamu wa ukuaji wa kiroho, saikolojia na maumbile; ya kwamba uovu humrudia mwovu.


Unaweza kutumia rushwa kutajirika lakini malipo ukayapata kupitia mgogoro wa ndoa na kudharaulika; ndiyo maana huwa sishangai ninapoona watu wengi wakitafuta furaha kupitia ngono na ulevi; wengi wao njia walizotumia kupata mafanikio waliyonayo zimewapa ‘garantii’ ya kutokuwa na furaha maisha yao yote!


Kwanini ninasema haya yote? Ni kwa sababu ninataka tuangalie upande wa pili kwamba tupende ama tusipende ni lazima wafanyakazi wote wafanikiwe ili kukabiliana na yanayowakabili maishani; lakini mnafanikiwaje? Ndipo hapo ninapotaka tuyaone maisha katika mwanga wa ujasiriamali.

Kila mfanyakazi anastahili kuishi maisha ya ushindi wa kiuchumi!

[email protected]

simu: 0719 127 901

By Jamhuri