Na Mwandishi Wetu ,Zanzibar

KATIBU Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar, Dkt. Mngereza Mzee Miraji, amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imepanga kuanza ujenzi wa Taasisi ya Saratani Zanzibar mwaka huu, ujenzi ambao unatarajiwa kukamilika ndani ya kipindi cha miaka miwili.

Taasisi hiyo inalenga kutoa huduma za matibabu ya saratani ndani ya Zanzibar, hatua itakayopunguza changamoto ya wananchi kusafiri nje ya visiwa hivyo kwa ajili ya matibabu, jambo ambalo limekuwa likiwagharimu muda na fedha nyingi.

Dkt. Miraji alitoa kauli hiyo baada ya kupokea ugeni kutoka Wakala wa Kimataifa wa Nguvu za Atomu duniani (IAEA), ugeni ulioongozwa na Bwana Gashaw Gebeyehu Wolde, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Ushirikiano wa Kiufundi kwa Afrika, pamoja na Bi. Azza Kashlan, Afisa wa Usimamizi wa Programu.

Kwa upande wake, Bwana Gashaw Gebeyehu Wolde alisema IAEA ipo tayari kushirikiana na Zanzibar kwa kupeleka wataalamu wa afya nje ya nchi kupata mafunzo maalum, ili wakirejea waweze kutoa huduma bora za matibabu ya saratani katika taasisi hiyo mpya.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania, Prof. Najat Kassim Mohammed, alibainisha kuwa ziara ya viongozi wa IAEA imelenga kutembelea miradi ya sekta ya afya na kilimo inayofadhiliwa na taasisi hiyo, ili kujionea maendeleo na namna inavyowanufaisha wananchi.