Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Morogoro

Ofisi ya Msajili wa Hazina (OMH), kupitia Kitengo cha usimamizi wa vihatarishi, imeanza kutoa mafunzo maalum kwa taasisi za umma kuhusu usimamizi wa vihatarishi na mpango wa kuendeleza shughuli za taasisi ‘Business continuity’ sambamba na matumizi ya mfumo mpya wa serikali wa GEMIS kwa ajili ya kuripoti taarifa za usimamizi wa vihatarishi.

Mafunzo hayo ambayo yanafanyika mkoani Morogoro kwa kipindi cha wiki mbili na kuhusisha taasisi 252 za umma, yanawalenga waratibu wa vihatarishi na mabingwa wa usimamizi wa vihatarishi pamoja na wataalamu wa mpango wa mwendelezo wa shughuli za taasisi.

Akizungumza Jumanne, Mei 19, 2026, Bi. Linah Igogo alisema mafunzo hayo yanalenga kuzijengea taasisi uwezo wa kuweka mikakati madhubuti ya kukabiliana na majanga au usumbufu wowote unaoweza kuathiri utekelezaji wa majukumu.

Alisema taasisi 252 ambazo ziko chini ya usimamizi wa OMH, zimegawanywa katika makundi manne, ambapo kila kundi litapatiwa mafunzo kwa muda wa siku tatu.

Bi. Igogo aliongeza kuwa dunia ya sasa imekuwa ikikumbwa na changamoto nyingi na majanga yanayoweza kuathiri shughuli za kila siku kwenye taasisi na uchumi kwa ujumla.

Alisema miongoni mwa changamoto hizo ni pamoja na migogoro ya kimataifa, majanga ya moto, mafuriko pamoja na changamoto za mtandao wa ‘internet’, ambazo zinaweza kusababisha kusimama kwa huduma muhimu katika taasisi mbalimbali.

Kutokana na hali hiyo, alisema Bi. Igogo, kuna haja kubwa kwa taasisi kujifunza namna ya kujiandaa na kuendelea kutoa huduma hata pale changamoto zinapotokea.

Kwa upande wake Ayubu Mswahili ambaye ni Mhadhiri kutoka Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA) na mtaalamu wa masuala ya usimamizi wa vihatarishi, alisema mafunzo hayo ni muhimu hasa katika kipindi ambacho dunia inakabiliwa na majanga mbalimbali kama vile mlipuko wa UVIKO-19 na changamoto nyingine.

“Taasisi zisipojiandaa mapema, zinaweza kushindwa kuendelea kutoa huduma wakati wa majanga”

Mswahili aliongeza kuwa uwepo wa mipango madhubuti ya mwendelezo wa shughuli za taasisi husaidia taasisi kuendelea kutoa huduma kwa muda hata wakati wa changamoto, wakati huo zikijiandaa kuendelea na shughuli kama kawaida.

Kwa kufanya hivyo, hii huongeza uaminifu kwa taasisi mbele ya wananchi na wadau, pamoja na kusaidia kujenga taswira nzuri ya taasisi katika mazingira yoyote.

Naye Mmoja wa washiriki kutoka Benki ya Biashara Tanzania (TCB), Maua Kibwana ambaye anafanya kazi katika Kitengo cha usalama wa mtandao na usimamizi wa mwendelezo wa Biashara alisema mafunzo hayo yana mchango mkubwa katika kuimarisha utoaji wa huduma za kifedha hasa wakati wa changamoto mbalimbali kama mafuriko au majanga mengine yanayoweza kuathiri shughuli za kila siku za taasisi.