Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Ruangwa
Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Ruangwa, Kaspar Mmuya, amezindua rasmi jengo la kupumzikia ndugu wa wagonjwa katika Hospitali ya Wilaya ya Ruangwa, mradi uliogharimu Shilingi milioni 35 kupitia Mfuko wa Jimbo la Ruangwa.
Mradi huo unalenga kuboresha mazingira ya utoaji wa huduma za afya kwa kuwapatia ndugu wa wagonjwa sehemu salama, yenye hadhi na inayowalinda dhidi ya jua, mvua na vumbi wanapokuwa wakisubiri wagonjwa wao kupata matibabu.
Akizungumza Agosti 3, 2026 wakati wa uzinduzi huo uliofanyika wilayani Ruangwa, Mhe. Mmuya amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kupeleka fedha za maendeleo zinazogusa mahitaji halisi ya wananchi kupitia Mfuko wa Jimbo na mifuko mingine ya maendeleo.
Amesema uamuzi wa kutenga Shilingi milioni 35 kwa ajili ya ujenzi wa jengo hilo ulitokana na changamoto iliyokuwa ikiwakabili ndugu wa wagonjwa waliolazimika kukesha nje ya hospitali katika mazingira yasiyo salama.
Aidha, amewataka viongozi na watumishi wa sekta ya afya kutunza miundombinu hiyo ili iendelee kutoa huduma kwa ufanisi na kunufaisha wananchi kwa miaka mingi ijayo.
Kwa upande wake, Kaimu Mganga Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa, Dkt. Msafiri Njaidi, amesema kukamilika kwa jengo hilo kutaboresha mazingira ya utoaji wa huduma kwa wagonjwa na ndugu zao kwa kuondoa changamoto ya kukosekana kwa sehemu salama ya kupumzikia.
Amesema jengo hilo pia litasaidia kupunguza msongamano katika maeneo ya kutolea huduma, hatua itakayochangia kuimarisha usafi wa mazingira na utekelezaji wa kanuni za kudhibiti maambukizi ya magonjwa mbalimbali.
Naye Kaimu Mtendaji wa Kata ya Nachingwea, Bi. Angel Mtengwa, amesema mradi huo ni ushahidi wa namna fedha za maendeleo zinavyoweza kutatua changamoto halisi za wananchi pale zinapotumika kwa ufanisi na kusimamiwa vizuri.
Amesema jengo hilo litawanufaisha wananchi wanaotoka maeneo ya mbali kwa kuwapatia sehemu salama ya kupumzika wanapokuwa wakisubiri ndugu zao wanaopatiwa matibabu katika Hospitali ya Wilaya ya Ruangwa.
Ujenzi wa jengo hilo ulianza Machi 12, 2026 na kukamilika kwa gharama ya Shilingi milioni 35 zilizotolewa kupitia Mfuko wa Jimbo la Ruangwa. Mradi huo ni sehemu ya jitihada za Serikali za kuendelea kuboresha huduma za afya na kuhakikisha wananchi wanapata huduma katika mazingira bora, salama na yenye utu.






