Mwaka 2013 nilichapisha chapisho la kitabu kinachoitwa ‘Lengo la Mpinga Kristo.’ Prudencia Onukwo, raia wa Kenya ni miongoni mwa wasomaji waliobahatika kusoma chapisho hilo. Prudencia alinitumia ujumbe mfupi kwa njia ya barua pepe, ujumbe huo aliupa jina la ‘Mwanadamu anaelekea kuzimu’.  Aliandika hivi: “Ole wetu kama dunia yetu itaacha kusali. Sote tutageuka na kuwa mashetani.” Ni kweli, dunia haiwezi kuwa salama bila sauti ya sala. Tusali bila kuchoka.

Sali ili uiokoe roho yako. Mtakatifu Alphonsus Liguori anasema: “Ukiwa mtu wa sala una uhakika wa kuiokoa roho yako. Lakini kama hausali unajiweka katika hali ya kuipoteza roho yako.” Kusali si kupoteza muda, bali ni kuutumia muda vizuri. Mtakatifu Augustino anathibitisha kwamba: “Anayejifunza kusali, anajifunza kuishi vema.” Kristo alinena dhahiri: “Bila mimi hamwezi kufanya lolote.” (Yh. 15:15).

Dunia inapita katika kipindi cha majaribu. Tunahitaji utambuzi wa kiroho kufahamu, majaribu, mwendo na mwelekeo wa ulimwengu huu. Dunia ya leo haitaki kusali, inaona sala inapoteza muda. Peter Marshall alisali hivi: “Tusamehe kwa kufikiria sala ni kupoteza muda na tusaidie tuone ukweli kuwa bila sala kazi yetu ni kupoteza muda.”

Inashangaza na kusikitisha kuona ulimwengu wetu sasa umegeuka kuwa uwanja wa maovu, hali ambayo inafifisha sana nguvu za watu kutafakari hatima ya maisha yao na uhusiano wao na Muumba wao. Unafika wakati ambao binadamu anajiuliza maswali mengi na pengine anashindwa kupata majibu ya maswali hayo na anashindwa kujua kwa nini, kwa sababu kwa kiasi kikubwa ni yeye mwenyewe ametengeneza mazingira yaliyozua maswali hayo.

Uhalisia wa jambo hilo ni huu: tunapotoka nje ya ndoa zetu na kufanya uzinzi, hatuko tayari kujikagua ili kuona ukweli wa jambo hilo na madhara yake, bali tunachoweza kufanya ni kuwasingizia wake au waume zetu kwamba wao ndio chanzo, kwa kigezo kwamba hawatujali. 

Tunapopata fedha na kuzitumia kwa matumizi mabaya hatujikagui na kujiuliza kama chanzo cha kufikia hatua hiyo ni sisi wenyewe, badala yake tunaanza kuwaambia wake zetu kwamba wana nuksi, pengine tunakwenda mbali kwa kuwasingizia jirani zetu kwamba wanakwenda kwa waganga wa kienyeji ili kutuharibia bahati.

Ni bahati mbaya kwamba watu wengi leo hii ni mafundi wakubwa katika mahusiano ya kidunia kwa njia ya simu, barua pepe, mitandao ya kijamii, magazeti, televisheni, redio na kadhalika. Lakini watu hao hao leo hii wanapuuza mawasiliano na Mungu wao. Wanamwendea Mungu wakiwa na mioyo nusu nusu. Wanamwendea Mungu wakiwa na matatizo. Wanamwendea Mungu wakiwa wanalalamika. Wanamwendea Mungu baada ya kukosa majibu ya matatizo yao.

Hii ni sawa na kwamba una jirani usiyemsalimia wala kujali uwepo wake lakini inapotokea una matatizo unamwendea ili akusaidie. Ndivyo tunavyomfanya Mungu wetu aliyetuumba kwa upendo mkubwa pasipo sisi kushiriki. Nia ni kuijenga dunia salama yenye watu salama. Hatuwezi kuijenga dunia yenye watu walio na mshikamano pasipo kumshirikisha Mwenyezi Mungu.

Kuna sauti ya uovu inasikika ulimwenguni. Sauti hii tuinyamazishe kwa kusali. Tuinyamazishe sauti ya kutoa mimba kwa kusali. Tuinyamazishe sauti ya ugaidi kwa kusali. Mwandishi Dwight Nelson katika kitabu chake cha ‘Passion of  Jesus’ anasema: “Watu wengi wanashangaa kwa nini Mungu hachukui hatua dhidi ya maovu yanayotokea ulimwenguni. Lakini Mungu anawashangaa Wakristo wake ni kwa nini hawasali kwa ajili ya yanayotokea ulimwenguni.” Tunasoma hivi katika Maandiko Matakatifu: “Mwenye kuvumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokoka.” [Mt. 10:23].  Tusali bila kuchoka tutaokoka.

“Bwana utufundishe kusali.” (Mt. 11:24).  Hili lilikuwa ni ombi la wanafunzi wa Yesu Kristo. Walimwomba Yesu Kristo awafundishe kusali. Yesu Kristo hakusita. Alilikubali ombi lao. Akawafundisha kusali (Mt. 6:9-13). 

Uhusiano wetu mzuri na Mwenyezi Mungu unajengwa kwa njia ya maisha ya sala. Mwandishi mashuhuri wa karne yetu, Giovan Papin, anasema: “Binadamu akitaka kusimama anahitaji kupiga magoti kwanza.” Sala ina nguvu katika maisha ya mtu binafsi, familia, taasisi na taifa.  Maisha yetu yawe ‘sala’. 

Mtawa wa Kanisa Katoliki, Carlo Carreto, ameandika: “Sala haiwezi kuwa bure hata mara moja.  Mimi ninaamini kwamba, hakuna kitu kiwezacho kuzuia nguvu ya sala.” Anayesali ni mtu wa thamani sana, ana moyo wa ajabu sana – uliojaa shukrani, upendo na mshangao, uliojaa furaha. Sala ni dawa ya kutu rohoni. Soren Kierkegaard anashuhudia kwamba: “Yule anayesali kwa unyofu wote wa moyo atabadili ulimwengu. Kama angekuwepo duniani mtu wa namna hiyo huwezi kuamini maajabu gani angeweza kutenda kutoka chumba chake cha sala.” Na St. Exupry anasema: “Ndani ya mtu anayesali kuna utajiri wa ajabu.”

By Jamhuri