*Barabara zenye changamoto kufikiwa

*Zipo barabara zenye kipaumbele kwa jamii

Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Singida

Mtendaji Mkuu wa Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) Mhandisi Victor Seff amewaagiza Mameneja wa Mikoa nchi nzima kuanza kutangaza  zabuni za mwaka wa fedha 2025/26.

Mhandisi Seff ameyasema hayo jana alipotembelea ofisi ya Meneja wa TARURA Mkoa wa Singida pamoja na kuzungumza na Mameneja wa TARURA wa wilaya katika mkoa huo.

“Tunatarajia kuanza kutangaza zabuni za mwaka 2025/2026 nchi nzima hivyo wiki ijayo maelekezo kuhusiana na mchakato wa ununuzi  zitatumwa  kwenu”.

Amesema katika zabuni hizo zizingatie barabara zenye kipaumbele kwa wananchi na zile zenye changamoto za kupitika

Pia Mtendaji Mkuu huyo aliwasisitiza Mameneja kufanya matengenezo ya barabara  kwa wakati na  kuhakikisha miradi yote ya kwenye maeneo yao inaanza mapema. 

Hata hivyo amewataka Mameneja wa wilaya kuandaa mipango ya kuboresha barabara kwa kuzingatia  vipaumbele.

Aidha, aliwataka kuandaa bajeti za matengenezo ya barabara kwa kila halmashauri kwa kuwa na mpango wa malipo kwa kutumia nguvu kazi.

Mhandisi Seff yupo Mkoani Singida ambapo jana tarehe 1 Mei, 2025 alishiriki katika Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi duniani na kupewa zawadi ya fedha na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  kwa kuwa Mfanyakazi hodari  wa TARURA kwa mwaka  2024/25.