Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Albert Chalamila ametoa shukrani hizo leo Agosti 28, 2023 katika ziara yake ya kutembelea na kukagua mradi wa Barabara Nzasa-Kilungule, Ujenzi wa Hospitali ya Ghorofa sita (6) na Ujenzi wa Soko la kisasa Mbagala Zakhiem.

RC Chalamila amesema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kipindi cha muda mfupi ameendelea kutoa pesa nyingi kwa ajili ya miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika maeneo mbalimbali ambapo hata miradi mikubwa iliyoachwa na mtangulizi wake Hayati Dkt John Pombe Magufuli hakuna mradi uliosimama.

Aidha RC Chalamila akiwa katika mradi wa Barabara ya Nzasa- Kilungule amesema mradi huo umetekelezwa katika Kipindi cha miaka miwili ya Dkt Samia lengo likiwa kukuza fursa za kiuchumi kwa wananchi, vilevile Mhe Rais ametoa fedha nyingi kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Ghorofa 6 na Soko la kisasa akiwa na dhamira ya kutoa huduma bora za afya kwa jamii na kuboresha mazingira ya wafanyabishara hususani wa eneo hili

Hata hivyo RC Chalamila amekemea vitendo vya uvunjifu wa amani kwani amani ikitoweka hakuna pahala pa kukimbilia, pia amekemea tamaduni za kimagharibi zinazoharibu jamii zetu kama vitendo vya Ushoga

Vilevile RC Chalamila ametoa rai kwa wanasiasa kushindana kwa hoja na sio kutumia lugha zisizo na staa, kwa upande wa katiba mpya ameitaka jamii kuwa makini katika mchakato huo kwa kuwa katiba nzuri ni ile yenye masilahi mapana kwa Umma na sio vyama vya siasa.

Mwisho RC Chalamila amezindua Soko la kisasa Mbagala Zakhiem na kuutaka uongozi wa Manispaa ya Temeke kusitisha zoezi la wafanyabishara kuanza kufanya biashara katika Soko hilo ili kujiridhisha watu waliopata vibanda katika Soko hilo tayari timu imeundwa ndani ya wiki moja kuanzia leo timu ifanye kazi kama kuna watu walikula pesa za watu kwa ahadi ya kuwapatia nafasi katika Soko hilo wazirudishe.