Chama cha ACT Wazalendo kimetaka hatua kali kuchukuliwa dhidi ya rais Donald Trump kufuatia hatua yake ya kutoa matamshi ya chuki dhidi ya mataifa ya Afrika na raia wanaotoka bara la Afrika.

Kulingana na gazeti la The Citizen ombi hilo lilitolewa na mkurugenzi wa kamati ya maswala ya kigeni katika chama hicho Vennace Msebo katika taarifa iliotolewa siku ya Jumamosi.

”Kwa niaba ya chama, ninashutumu pakubwa matamshi ya ubaguzi wa rangi ya rais Donad Trump.Kuwaita Waafrika na watu kutoka Afrika wachafu ni ubaguzi wa rangi na tabia ya chuki ya utawala mpya wa Marekani kwa bara Afrika na ulimwengu hautanyamaza”, alisema.

Aliongezea: Tunapongeza hatua ya taifa la Botswana kuhusu swala hilo na tunajivunia kwamba taifa la Botswana limekuwa katika mstari wa mbele katika kushutumu kwa vitendo swala lolote linalokandamiza Afrika na watu wake.

Kwa mujibu wa gazeti hilo aliongezea kwamba ”vilevile tunapongeza taarifa iliotolewa na mwenyekiti wa muungano wa Afrika na hatua iliochukuliwa na mabalozi wa Afrika mjini Washington na tunaunga mkono hatu hiyo.

Aidha ameyataka mataifa ya bara Afrika kutathmini matamshi hayo ya rais wa Marekani kama muamko kwa mataifa ya Afrika ili kujiimarisha kiuchumi na kukabiliana na umasikini kwa lengo la kujisimamia.

 

By Jamhuri