Hapa nchini Tanzania nadhani hata huko ughaibuni kwenye nchi zinazojulikana kama za ulimwengu wa kwanza, wananchi wanazungumzia uwepo wa vyama vya siasa na demokrasia.

Vyama vyenyewe kwa asili yake vilianza wapi na vilianza namna gani katika nchi zile, haijaelezwa wazi. Wale wenzetu walioendelea kule Magharibi bado wanaamini wana wajibu wa kuviangalia vyama vya siasa katika nchi huru za Afrika.

Ndiyo sababu kukiwa na uchaguzi mkuu katika nchi huru zote za Afrika, utasikia kuwa tume za uangalizi kutoka Umoja wa Mataifa (UN) au Umoja wa Ulaya (EU), wanaoitwa “international observers” wanatumwa kuja kuangalia namna demokrasia wanaoijua wao imekua kwa kiasi gani.

Kwa nchi zetu za Kiafrika ndiyo hasa hivyo vikundi vinakuwa vingi. Mathalani kule Zimbabwe; Julai 30, mwaka huu kulikuwa na waangalizi (observers) kutoka nchi huru za Afrika (AU), Umoja wa Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADAC), EU na UN.

Loo! “Observers” wote hawa wa nini? La msingi, demokrasia katika nchi zinazoendelea haiaminiki! Hivyo, waliobobea katika suala la demokrasia lazima waje wathibitishe. Basi, wanajiona kama vile wana wajibu wa kuja kuangalia sisi tusioendelea tunafanyaje.

Mbona ulipotokea uchaguzi mkuu kule Marekani, kati ya Bibi Clinton na tajiri Trump suala hili la “International Observers” halikuwapo? Kumekuwa na uchaguzi Ufaransa (2017) na kule Urusi (2018) au Ujerumani (2018) na Italia (2017) mbona haikusikika wametumwa waangalizi kutoka AU, au EU au UN? Ndiyo kusema huko kwa wenzetu waangalizi hawahitajiki? Kama hivyo ndivyo, tujiulize kwanini hawa “International Observers” hawahitajiki kule, lakini wanahitajika huku kwetu Bara la Afrika?

 

Basi hiki ni kisasili (myth) tu kimejengeka miongoni mwa wakubwa- Wazungu hawa. Kuwa demokrasia kwao haina dosari maana imeanza huko, sisi tuliletewa tu na wakoloni na hivyo lazima waisimamie wao. Nasi kwa unyonge wetu “inferiority complex” tukaipokea hali ile mpaka leo hii.

Azimio la Arusha linasema, “…Tumeonewa kiasi cha kutosha, Tumenyonywa kiasi cha kutosha na Tumepuuzwa kiasi chakutosha…”

“…unyonge wetu (inferiority complex) ndiyo uliotufanya tuonewe, tunyonywe na kupuuzwa…Si ndio hayo tunayoyaona sasa toka kwa Wazungu?

Lakini kule nchi za Ulaya na Marekani hii democrasia, na mambo ya vyama vya siasa viliibukaje? Nani aliwapa hawa Wazungu hati miliki ya demokrasia ambayo kwao wanaamini lazima watufundishe sisi na kutusimamia?

Hili Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere aliita “Jeuri ya Kikoloni”. Hebu jaribu kusoma tena ile hotuba ya Mwalimu Nyerere aliyotoa Dar es Salaam Siku ya Kumbukumbu ya Uhuru wa Tanganyika tarehe 09 Desemba, 1978 wakati tukiwa katika maandalizi ya vita ya kumng’oa nduli Idd Amin kutoka Kagera. Hotuba ile sasa ni wakati muafaka kuitafakari.

Mimi nimeonelea ni vema sasa tuelimike juu ya hii “demokrasia” na juu ya vyama vya siasa namna vilivyoanzishwa ulimwenguni na hizo jeuri za wakoloni waliotutawala na bado wanajifikiria kusimamia demokrasia katika nchi huru zinazoendelea ulimwenguni.

Historia inatueleza waziwazi kuwa neno “Demokrasia” na “Vyama vya Siasa” asili yake ni Ugiriki ile ya zamani kabla hata ya kuzaliwa kwa Bwana wetu Yesu Kristo kipindi kihistoria kinaitwa BC (Before Christ) yaani Kabla ya Kuzaliwa kwa Kristo). Ni karne kwa karne za hiyo BC.

 

Enzi hizo Wagiriki waliibuka kuwa taifa la majitu ya kufikiri sana – wanafalsafa wakubwa na wanasayansi kweli kweli. (Great phylosophers and scientists). Tunayakuta majina mashuhuri kama Aristotle (384 – 322 BC) mwana sayansi mahiri wa Athens enzi hizo, Plato – 400 BC (mshairi maarufu); Socrates (470–399BC) -mwanafalsafa wa Athens.

Archimedes (287–242BC) aliyebobea katika hesabu na akatugundulia ile kanuni maarufu katika fizikia inayoitwa kanuni ya “Ueleaji Majini” (Principle of Floatation). Mimi bado nakumbuka lile neno la Kiyunani alilolitamka huyu Archimedes “Eureka – Eureka” akimaanisha “nimegundua, nimegundua”, hiyo kanuni ya kuelea. Nadhani wasomi wote wa elementary physics wanajua hili.

Lakini kuna Mgiriki mwingine anaitwa Solon (640BC) huyu inasemekana alikuwa mwanasheria. Ulizuka mzozo kati ya vikundi viwili mjini Athens enzi hizo. Basi, aliombwa kuwa “umpire” yaani msuluhishi au mpatanishi katika vikundi vile viwili kule Athens. Hakupenda kuitwa mtawala, bali alisema yeye alikuwa kiongozi wao kwa vile alivyomaliza mzozo ule uliozuka kati ya wanyonge (Oppressed poor class) na mabwanyenye wenye ardhi (powerfull aristocratic families) waliowakodisha wanyonge wale vihamba vya kulima na viwanja vya kujenga nyumba (plots) kwa gharama au kodi kubwa.

 

Inasemekana kati ya mwaka 594/593 Mgiriki huyu Solon alibuni njia au namna ya kuzungumzia matatizo ya wananchi wale wa Athens. Njia ile ilikuwa ni KIKAO cha pamoja kuzungumzia matatizo ya wanyonge na mabwanyenye – katika kutafuta usuluhisho. Yeye aliita njia ile “Ekklesia”, maana yake “Kikao”. Pale walikutana makundi yote mawili (wanyonge) makabwela na mabwanyenye (waliokuwa matajiri). (Tazama Encyclopaedia Britannica Vol. 20 Uk. 954-955).

Kwa vile haingewezekana kabwela wote wa Athens na mabwanyenye wote wakutane pale “Ekklesia” ndipo Solon akabuni namna ya makundi yale mawili kuchagua wawakilishi wao ambao ndio watakaowajibika kufika pale “Ekklesia” (kikaoni) na kuongelea mambo yao mpaka kupatikane suluhisho kwa pande zote mbili.

Basi, kwa mantiki ya Wagiriki wale chini ya uongozi wa Solon, waliona kwa sasa wamepata MFUMO wa kutatua mambo yao kupitia ile “Ekklesia” ambako wajumbe wao waliochaguliwa kutoka makundi mawili tofauti (yanayopingana kimaslahi). Sasa waliweza kukaa na kuchambua na hatimaye kupata ufumbuzi au suluhisho la matatizo yao.

Sera ile sasa waliita “DEMOKRASIA” na kwa Kigiriki neno lile linatokana na maneno mawili ya Kigiriki. Neno “DEMOS” likiwa na maana ya WATU, na neno “KRATOS” likiwa na maana ya nguvu. Sasa kwa kuunganisha yale maneno mawili ndipo likapatikana neno moja hilo DEMOKRATIAmaana yake NGUVU YA WATU (The Power of People) kwa maana hiyo Ekklesia ile ilikuwa na maana kikao kinachoendeshwa na watu waliochaguliwa na wananchi wenyewe kutatua kero zao wananchi wenyewe kimaslahi na ya kipaumbele.

Kuanzia hapo ndipo kukazuka huu utaratibu wa uchaguzi wa wawakilishi wa watu upande wa mabwanyenye na upande wa makabwela. Upande mmoja au kikundi kimoja kinatetea maslahi yake wakati kundi jingine au upande mwingine nao unatetea maslahi yake pia. Kabwela walikuwa na wawakilishi wao na mabwanyenye walikuwa na wawakilishi wao. Itikadi ya kila kikundi ilikuwa kutetea maslahi ya kundi lao huko kwenye Ekklesia. Hii ITIKADI ndiyo SERA YA SIASA ya kila upande.

 

Kule kutetea maslahi ndio SIASA yenyewe na ndio ITIKADI yenyewe ya chama. Huo basi mimi nafikiri kuwa ndio mwanzo haswa wa VYAMA VYA SIASA ulimwenguni.

Waingereza wao wakanyambua lile neno “DEMOKRATIA” kwa lugha yao ikawa “democracy is a form of government of the people for the people and by the people”

Sisi kwa Kiswahili tukalitafsiri kutoka kwa Waingereza tukasema DEMOKRASIA ni mfumo wa serikali ya watu kwa ajili ya watu na imetokanana watu.

Kuanzia pale au kule Ugiriki miaka hiyo ya BC Kabla ya Kuzaliwa kwa Bwana wetu Yesu Kristo mpaka leo hii kila taifa linajidai linatumia demokrasia katika utawala wake. Wamenyambua na kutafsiri kivyao lile lile neno la Kigiriki la “Demokratia”.

 

Kadri miaka ilivyokwenda mfumo wa ile “Ekklesia” nao ukawa unabadilika. Tunaambiwa na wanahistoria kuwa mpaka kwenye karne ya 17 huko (miaka ya 1600 AD – yaani Anno Domin mwaka wa Bwana baada ya kuzaliwa kwa Kristo) ulimwenguni hapakuwapo kitu kinachoitwa au kinachojulikana kama CHAMA CHA SIASA tangu kule enzi za Wagiriki.

 

Itaendelea….

By Jamhuri