Jamhuri Media, Tel Aviv

Bibi mstaafu Rahel Idri alishikiliwa kwa bunduki na wapiganaji wa Hamas kwa saa 20 nyumbani kwake, lakini alitumia chakula na mazungumzo kuwavuruga hadi msaada ulipowasili. Idri alialikwa kukutana na Rais wa Marekani Joe Biden wakati wa ziara yake nchini Israel.

“Mmoja wa magaidi hao aliniambia: Unanikumbusha mama yangu,” anakumbuka Rahel Edri.

“Nilimwambia, ‘Mimi ni kama mama yako. Nitakusaidia: nitakutunza. Unahitaji nini?”

Jibu lilikuwa chai na biskuti.

Bibi huyo mstaafu mwenye umri wa miaka 65 aliwahudumia keki zake za Morocco ili kuwatuliza wanajeshi watano wa Hamas waliovamia nyumba yake huko Ofakim, mji ulio karibu na Gaza.

Mazungumzo hayo yalirefusha muda hadi yeye na mumewe walipopata usaidizi aliviambia vyombo vya habari vya Israel.

Mazungumzo hayo ya kawaida yalimaanisha mengi.

Wakati wanajeshi wa Hamas walipowakamata mnamo Oktoba 7, makumi ya watu walikuwa tayari wameuawa katika jamii yake kusini mwa Israeli.

Kutokana na subira na ukarimu wake, yeye na mume wake walinusurika, na Rahel akawa shujaa wa kitaifa, hata kukutana na Rais wa Marekani Joe Biden wakati wa ziara yake huko Tel Aviv.

Nyimbo za Kiarabu na Kiebrania

Katika mahojiano ya televisheni, alizungumza kuhusu mazungumzo aliyokuwa nayo na askari watano wenye silaha nzito waliokuwa wameketi sebuleni kwake.

“Ilikuwa tayari saa nne.” Nikajiambia: Oh my…lazima wapate chakula cha mchana. Ninaogopa, watu walio na njaa wanashindwa kujizuia,” alisema.

“Kwa kuwa walikuwa wakinywa na kula, walitulia,” aliongeza.

Lakini chai na biskuti havikuwa vyote ambavyo Idri alitoa kwa wanamgambo waliomshikilia yeye na mumewe kwa mtutu wa bunduki kwa saa ishirini.

Aliwaimbia nyimbo kwa Kiarabu, na walijibu kwa nyimbo za Kiebrania, anasema.

“Nilianza kuzungumza nao na kwa muda nilisahau kwamba walikuwa magaidi,” Idri aliambia tovuti ya habari ya Israel, Inet.

Ujumbe wa uokoaji

Wakati huo huo, timu ya polisi wa Israel ilikuwa ikijiandaa kuwaokoa.

Karibu saa kumi na moja jioni, waliingia ndani ya nyumba na kuwaua wanamgambo hao.

Mtoto wa Rahel Idri – mwenyewe ambaye ni polisi wa eneo hilo – alisaidia katika uokoaji kwa kuchora mchoro wa nyumba, kuruhusu waokoaji kuwavamiz wanamgambo.

Kwa kuwa nyumba hiyo ilikuwa imeharibika vibaya, Idri na mumewe walipelekwa katika hoteli moja katikati mwa Israeli.

Hadithi ya Rahel Idri jasiri ilianza kuenea zaidi ya mipaka ya Israeli, na Rais wa Marekani Joseph Biden alipokutana na manusura, bibi huyu alikuwa miongoni mwao.

Alitabasamu sana huku akimkumbatia Rais wa Amerika, na akamshukuru kwa “kutetea nchi”… kwa chai, biskuti na mazungumzo ya kutuliza.

“Naomba ulimwengu umlete mtoto wangu nyumbani”

“Naomba ulimwengu umlete mtoto wangu nyumbani”

Chanzo: BBC Swahili.

By Jamhuri