Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Albert Chalamila leo Septemba 22,2023 ametembelea kiwanda cha Kisasa cha Elsewedy kinachozalisha vifaa vya Umeme kilichoko Kisarawe II Kigamboni Jijini Dar es Salaam.

lbert Chalamila akiwa katika kiwanda hicho amepata wasaa wa kuona mitambo mbalimbali ya kisasa ambayo hutumika kuzalisha vifaa vya Umeme ikiwemo Transformers, nyaya za umeme na vifaa vingine vingi vya Umeme ambayo vinazalishwa kwa teknolojia ya hali ya juu na ubora unaokidhi viwango vya ushindani katika Soko la ndani na nje.

Aidha RC Chalamila amesema ziara yake katika kiwanda hicho imelenga kujionea namna kiwanda hicho kinavyofanya kazi lakini pia kuona Changamoto zinazo wakabili wawekezaji kwa kuwa ukanda wa kisarawe II ni ukanda wa viwanda hivyo lazima kuwe na Barabara za Lami, maji ya kutosha vilevile Umeme.

Kutokana na dhamira njema ya Rais Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan ameendelea kuwekeza kiasi kikubwa katika uboreshaji wa miundombinu ya barabara tayari ametoa pesa za kujenga Barabara ya Kisarawe II Kilomita 41 kwa kiwango cha lami hiyo haitoshi anaendelea kuboresha miundombinu ya Maji kupitia DAWASA na Umeme ili eneo hilo liwe rafiki kwa wawekezaji kwa masilahi mapana ya Mkoa na Taifa kwa Ujumla.

Sambamba na hilo RC Chalamila amesema Elsewedy Electric Factory ni mwekezaji anayetoa ajira kubwa kwa Watanzania pia ni mlipaji kodi mzuri hivyo Serikali inaendelea kukaribisha wawekezaji wa aina hiyo kwa masilahi mapana ya watu wengi hususani Watanzania.

Ifahamike kuwa kiwanda cha Elsewedy ni miongoni mwa uwekezaji mkubwa katika ukanda wa kisarawe II ambao unafungua fursa za kiuchumi kwa wakazi wa Kigamboni, Mkoa wa Dar es Salaam na Tanzania kwa ujumla hivyo hatuna budi kuunga mkono kazi nzurii inayofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan.