Na. Benny Mwaipaja, Zanzibar
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), ameimwagia sifa Mamlaka ya Mapato Tanzania-TRA kwa utendaji uliotukuka uliowezesha Mamlaka hiyo kuendelea kuvuka malengo ya ukusanyaji wa mapato kila mwezi na kueleza imani yake kwamba kwa kushirikiana na alipakodi, wataweza kuvuka lengo walilopangiwa la kukusanya zaidi ya shilingi trilioni 42 katika Mwaka wa Fedha 2026/2027.
Mhe. Balozi Omar, ametoa pongezi hizo wakati wa hafla ya uwekaji wa Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Jengo la Ofisi ya TRA, Kizimkazi, Zanzibar, litakalokuwa na ghorofa moja, ambapo hadi kukamilika kwake linatarajiwa kugharimu shilingi bilioni 3.6.
Sifa hizo kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania-TRA, zinafuatia maelezo ya Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania-TRA Bw. Yusuph Mwenda ambapo alisema katika mwezi Julai mwaka huu, Mamlaka yake imevuka malengo kwa kukusanya shilingi trilioni 3.2 ikilinganishwa na malengo waliyopangiwa ya kukusanya shilingi trilioni 2.
Alisema kuwa mafanikio ya TRA katika ukusanyaji wa mapato yanatokana na ushirikiano wa karibu kati ya Serikali, Bunge na wadau wa kodi, ambapo mwezi Julai pekee, Mamlaka ilikusanya zaidi ya Shilingi trilioni 3.245 ikilinganishwa na lengo la mwezi la kukusanya shilingi trilioni 2.971, sawa na ufanisi wa asilimia 109 ya lengo, na ukuaji wa asilimia 21.
“Kutokana na usimamizi wako mzuri Mhe. Waziri wa Fedha, na ushirikiano na walipakodi, tunakuhakikishia tutavuka lengo hilo na kupita, ishara inayoonesha kwamba tumeanza mwaka wa fedha kwa nguvu kubwa, na tuna imani tutafikia na kuvuka malengo tuliyowekewa” alisema Bw. Mwenda.
Aidha, CPA Mwenda alisema kuwa katika kipindi hicho cha Julai, 2026, TRA imefanikiwa kukusanya shilingi bilioni 325, fedha mabazo ni asilimia 70 ya makusanyo yote na kuzipeleka moja kwa moja kwenye Mifuko 11 ya ujenzi wa miundombinu katika sekta mbalimbali zikiwemo Barabara, maji, utalii na sekta nyingne.
Akizungumzia kuhusu ujenzi wa Ofisi za TRA, Kizimkazi-Unguja Zanzibar inayojengwa na Kampuni ya CRJE ya China, ni sehemu ya ujenzi wa Ofisi kama hizo 49 zinazojengwa nchi nzima zikitarajiwa kugharimu zaidi ya shilingi bilioni 32 kwa ajili ya kuboresha mazingira ya ulipaji kodi na kusogeza huduma karibu na wananchi.
Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) aliwahakikishia watanzania kuwa Serikali imejipanga kuhakikisha kuwa inajitegemea kwa kutumia mapato yake ya ndani kutekeleza miradi yake ya maendeleo ambapo katika Mwaka wa Fedha 2026/2027, imepanga kujitegemea kwa zaidi ya asilimia 74.
Alisema kuwa ujenzi wa Ofisi za TRA Kizimkazi na maeneo mengine nchini, ni mikakati ya Serikali ya kuimarisha huduma, kurahisisha shughuli za biashara, kuongeza ufanisi katika ukusanyaji wa mapato na kuwawezesha watumishi kufanya kazi katika mazingira bora kwa ajili ya kuongeza mapato yanayowezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo ikiwemo barabara, nishati, maji, kuimarisha huduma za afya na kuwekeza katika elimu.
Mhe. Balozi Omar ameuagiza Uongozi wa TRA kuhakikisha kuwa wanashirikiana na Mamlaka ya Mapato Zanzibar ZRA kutumia miundombinu ya Ofisi hizo na nyingine zitakazo jengwa Visiwani Zanzibar, ili wadau wa kodi wapate huduma kikamilifu, jambo ambalo Kamishna wa TRA Bw. Mwenda aliahidi kulifanyia kazi.
Aidha aliwataka wafanyabiashara na wananchi kutimiza wajibu wao wa kulipa kodi kwa wakati, kwa ukamilifu na kwa hiari, akisisitiza kuwa ulipaji wa kodi unapaswa kuwa jambo la fahari kwa kila mwananchi anayewajibika na Serikali itaendelea kushirikiana na wafanyabiashara katika kuboresha huduma za kodi na kupunguza changamoto zinazowakabili, huku ikitarajia wafanyabiashara nao kutimiza wajibu wao wa kulipa kodi.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Kusini Mkoa wa Kusini, Mhe. Othman Ali Maulid, alitoa wito kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Mamlaka ya Mapato Zanzibar (ZRA) kuendelea kuimarisha ukusanyaji wa mapato kwa ufanisi na kuzingatia utoaji wa huduma bora kwa wananchi, lakini pia kusikiliza changamoto za wananchi na wafanyabiashara.
Akiongea kwa niaba ya Wafanyabishara wa sekta ya hoteli na utalii Zanzibar, Bw. Henry Kaunda, aliishukuru TRA na ZRA kwa kushirikina na wafanyabiashara na kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili hatua iliyochangia ulipaji kodi kwa hiari na kuomba elimu zaidi ya mlipakodi iendelee kutolewa kwa wafanyabiashara.



