Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imeteketeza ekari 603 za mashamba ya bangi na kukamata magunia 49 ya bangi katika operesheni maalum iliyofanyika Wilaya ya Mvomero, mkoani Morogoro, huku watuhumiwa 13 wakikamatwa kuhusisiana na mashamba hayo.
Operesheni hiyo iliyofanyika katika vijiji vya Misengele, Lugenge, Kisaki na Nyarutanga, pia ilibaini na kuharibu kambi 21 zilizokuwa zikitumiwa na wakulima wa bangi.
Akizungumza kuhusu operesheni hiyo, Kamishna Jenerali wa DCEA Aretas Lyimo, amesema hatua hiyo ni sehemu ya mkakati endelevu wa Serikali wa kudhibiti uzalishaji wa dawa za kulevya nchini, hususan bangi, ambayo imeendelea kuzalishwa katika baadhi ya maeneo ya nchi.
Amesema operesheni hizo zimebaini mabadiliko katika mbinu zinazotumiwa na baadhi ya wakulima wa bangi, ambapo wanahamisha shughuli zao kutoka maeneo yaliyofikiwa na operesheni na kuingia ndani zaidi ya maeneo ya hifadhi.
“Tumebaini kuwa baadhi ya wakulima wamehamishia shughuli zao ndani zaidi ya maeneo ya hifadhi ili kukwepa hatua za kisheria. Hali hii inachangia uharibifu mkubwa wa mazingira kupitia ukataji wa miti ovyo, uvamizi wa vyanzo vya maji na kuathiri mfumo wa ikolojia,” amesema Lyimo.
Kwa mujibu wa Lyimo, tathmini ya operesheni zilizotekelezwa na DCEA tangu mwaka 2023 imeonyesha kuwa, licha ya mashamba mengi ya bangi kubainika na kuteketezwa katika Mkoa wa Morogoro, baadhi ya wahusika wameendelea kubadilisha maeneo ya uzalishaji na kujificha ndani ya maeneo ya hifadhi.
Amesema hali hiyo inahitaji ushirikiano wa karibu zaidi kati ya DCEA, vyombo vya ulinzi na usalama, mamlaka zinazosimamia maeneo ya hifadhi na wananchi ili kuzuia maeneo hayo kutumiwa kwa uzalishaji wa dawa za kulevya.
Lyimo amewataka wasimamizi wa maeneo ya hifadhi kuhakikisha maeneo wanayoyasimamia hayatumiki kwa kilimo cha bangi, akisisitiza kuwa mapambano dhidi ya uzalishaji wa dawa za kulevya yanahitaji ushirikiano wa taasisi na jamii.
DCE itaendelea kufanya operesheni jumuishi katika maeneo mbalimbali nchini kwa kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama, mamlaka za uhifadhi na wananchi ili kudhibiti kilimo na biashara haramu ya bangi.
Sambamba operesheni hizo, Lyimo amesema Mamlaka itaendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu madhara ya dawa za kulevya na kuhamasisha wananchi kutoa taarifa kuhusu watu wanaojihusisha na uzalishaji, usafirishaji na biashara haramu ya dawa za kulevya.


