Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi amesema kuwa Ilani ya Uchaguzi ya CCM 2020-2025 imeelekeza kujenga kilomita 200 za barabara hadi sasa Serikali imejenga kilomita 800 kwa kuvuka malengo ya ilani hiyo.

Rais Dk.Mwinyi amesema hayo alipofungua Barabara ya maeneo huru ya kiuchumi Wilaya ya Micheweni, Mkoa wa Kaskazini Pemba tarehe 23 Aprili 2024 ikiwa ni mwendelezo wa shamrashamra za Miaka 60 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

Aidha Rais Dk.Mwinyi amesema baada ya muda mfupi Pemba itafunguka kiuchumi kwa uwekezaji, viwanda, ujenzi wa uwanja mpya wa ndege, ujenzi wa barabara ya Chakechake hadi Mkoani na Chakechake hadi Wete, ujenzi wa bandari ya shumba na kukamilika bandari ya Mkoani.

Halikadhalika Rais Dk.Mwinyi amesema Serikali itawasimamia wawekezaji kuajiri vijana wazawa wa eneo hilo.

Rais Dk.Mwinyi amesema atawashawishi wawekezaji wengi zaidi kuanzisha viwanda vya kuchakata mazao ya bahari katika maeneo hayo.

Kwa upande mwingine Rais Dk.Mwinyi amesema nchi ina amani na utulivu kwa sababu ya Muungano uliopo na kuendelea kupiga hatua za maendeleo, amewataka wananchi kuudumisha.

Vilevile Rais Dk.Mwinyi amemkabidhi Omar Hassan mkazi wa MaziwaNg’ombe usafiri wa miguu mitatu(Bajaj) ikiwa ni utekelezaji wa maombi yake wakati wa ziara yake Januari mwaka huu.

By Jamhuri