IGP Wambura awataka askari kutenda haki

Na Mwandishi Wetu,JamhuriMedia,Kilimanjaro

Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Camillus Wambura amewataka askari wa Jeshi hilo kuzingatia uadilifu na kutenda haki wakati wanapo wahudumia wananchi kwa kufanya kazi kwa weledi ili kufikia malengo ya kulinda watu na mali zao.

IGP Wambura amesema hayo wakati akifungua kituo cha Polisi Ngoyoni kilichopo Rombo mkoani Kilimanjaro ambapo mbali na kutoa pongezi kwa wadau werevu waliofanikisha ujenzi wa kituo hicho pia amewataka wananchi kujiepusha na utengenezaji wa pombe ya moshi aina ya gongo, kujiepusha na matukio ya mauaji yanayotokana na migogoro ya ardhi sambamba na mauaji yanayotokana na wivu wa mapenzi.

Naye Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro ACP Simon Maigwa amesema kuwa, ujenzi wa kituo cha Polisi Ngoyoni hadi kukamilika kwake unatarajiwa kugharimu kiasi cha shilingi milioni 128 ambapo kitarahisisha utoaji wa huduma za Kipolisi kwa kushughulikia makosa mbalimbali ikiwemo uhalifu na wahalifu.

Akizungumza kwa niaba ya familia ya Assenga Bi. Catheline Assenga amesmea kama familia wameridhia kutoa kwa hiari eneo walilokuwa wakimiliki na kulikabidhi kwa Jeshi la Polisi ili kujenga kituo cha Polisi kwenye eneo hiyo.