Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia

Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo Hospitali ya Taifa Muhimbili Mloganzila Dkt. Fabian Kamana ametoa rai kwa jamii kupunguza matumizi ya mafuta, chumvi, sukari, tumbaku na pombe kwa wingi kwa kuwa vyote hivi husababisha mtu kupata magonjwa yasiyoambukiza ikiwemo magonjwa ya moyo .

Dkt. Kamana amesema maradhi ya moyo yanaweza kuepukika endapo jamii itabadili mtindo wa maisha kwa kufanya mazoezi na kula chakula wa kuzingatia ushauri wa wataalamu wa lishe.

“Pia ni vizuri jamii ikajenga utamaduni wa kufanya uchunguzi wa afya zao mara kwa mara ili iweze kujua hali za afya zao mapema, hii itasaidia kuchukua hatua kwa wakati kwakuwa maradhi haya yakipata matibabu mapema inaweza kusaidia kuepuka madhara makubwa kujitokeza” amefafanua Dkt. Kamana.

Dkt. Kamana ameongeza kuwa dalili za magonjwa ya moyo ni pamoja na mtu kuvimba miguu, mwili kuchoka, maumivu ya kifua, kichwa kuuma na mapigo ya moyo kwenda kasi isivyo kawaida.

Dkt. Kamana amebainisha kuwa kwa mujibu wa chapisho ya Shirika la Afya Duniani WHO la mwaka 2015, watu milioni 17.7 duniani hupoteza maisha kwa mwaka kutokana na matatizo ya moyo na inakadiriwa kuwa hadi kufikia 2030 wataongezeka kufikia milioni 23 na kundi linaloathirika ni wenye umri wa kati ya miaka 25 hadi 65.

Aidha chapisho la WHO la mwaka 2017 linaonesha kuwa takribani asilimia 13 ya Watanzania hupoteza maisha kwa mwaka kutokana na maradhi hayo, ambapo kwa siku MNH -Mloganzila inahudumia wagonjwa wa moyo 30 hadi 50 kwa siku.

Dkt. Kamana amesema madhara ya magonjwa ya moyo ni pamoja na kupata ugonjwa wa kiharusi au moyo kushindwa kufanya kazi kabisa na hatimaye inaweza kusababisha vifo.

MNH-Mloganzila inatoa huduma ya kliniki ya magonjwa ya moyo kila siku ya Jumatatu hadi Ijumaa Saa 2:00 Asubuhi hadi saa 11:00 Jioni, kliniki hii inapatikana ghorofa ya kwanza ambapo kuna wataalamu na mashine za uchunguzi na za kisasa.

By Jamhuri