Mahakama ya Hakimu Mkazi Wilaya ya Igunga mkoani Tabora imemuhukumu Daudi Masanja (28), mkazi wa mtaa wa Masanga, Kata ya Igunga mjini kutumikia kifungo cha maisha jela baada ya kutiwa hatiani kwa kosa la kulawiti wanafunzi wawili wanaosoma shule msingi Azimio kata ya Igunga.

Ametoa jana adhabu hiyo Hakimu Mfawadhi wa Wilaya ya Igunga, Lydia Ilunda amesema kwamba hukumu hiyo itakuwa fundisho kwa watu wengine wenye nia ovu kama aliyofanya mshitakiwa .

Amesema kwamba ili kukomesha vitendo vya kuwadhalilisha watoto wadogo mahakama itakuwa inatoa adhabu kali .

Lydia amesema ushahidi uliotolewa na upande wa Jamhuri Mahakama imeridhika nao pasipo shaka, hivyo mahakama imemuona mshtakiwa ana hatia.

Amesema Mahakama inaungana na upande wa mashitaka hivyo mshitakiwa kwa makosa yote mawili ya kulawiti Mahakama inamuhukumu kutumiki kifungo cha maisha gerezani ili iwe fundisho kwa wengine wenye tabia kama hiyo.

Awali, Mwendesha mashtaka wa Serikali kutoka Wilaya ya Igunga Grace Lwila akimsomea mashitaka mawili ya kulawiti mshtakiwa huyo mbele ya Hakimu Mfawadhi wa wilaya ya Igunga Lydia Ilunda.

Ameiambia Mahakama kuwa Mshtakiwa Daudi Omari Masanja ametenda makosa hayo mawili Mei 16,2023 majira ya mchana katika Mtaa wa Masanga Kata ya Igunga mjini.

Amesema katika tarehe hiyo na muda huo alimlawiti mwanafunzi wa miaka 13 anayesoma darasa la sita shule ya msingi Azimio hata hivyo baada ya kumfanyia kitendo hicho alikwenda kwa mwanafunzi mwingine wa miaka 8 anayesoma darasa la tatu katika shule hiyo ya msingi Azimio.

Mwendesha mashtaka huyo aliendelea kuiambia Mahakama kuwa mshtakiwa Daudi alitenda makosa hayo mawili kinyume na kifungu 154 A cha kanuni ya adhabu sura ya 16 mapitio ya mwaka 2022 inayozuia kutenda makosa kama hayo.

Hata hivyo baada ya kusomewa mashitaka hayo mawili mshtakiwa huyo alikana kutenda makosa hayo yote na ndipo upande wa Jamhuri ulipeleka mashahidi 8 Mahakami wakiwemo waathilika hao pamoja na daktari ambao kwa nyakati tofauti wote walitoa ushahidi mahakamani wa kumtambua mshitakiwa.

Aidha kabla ya mahakama kutoa adhabu kwa mshitakiwa mwendesha mashitaka wa Serikali Grace Lwila aliomba mahakama kutoa adhabu kali kwa mshitakiwa kwa kuwa kitendo alichofanya mshitakiwa huyo ni cha aibu na kimeleta fedheha kwa jamii na Taifa kwa ujumla.