Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Angellah Kairuki amebainisha vipaumbele na maeneo ambavyo Wizara itawekea mkazo katika kipindi ambacho atakuwa akihudhumu katika Ofisi ya Rais TAMISEMI.

Amebainisha hayo leo tarehe 03 Novemba, 2022 wakati alipopewa nafasi na Spika wa Bunge, Mhe. Dkt. Tulia Ackson kutoa salamu kwa Wabunge wakati wa mkutano wa tisa, kikao cha tatu cha Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Waziri Kairuki amesema atashirikiana na viongozi wa Wizara hiyo kuweka mifumo endelevu ya kitaasisi ambayo itaendelea kudumu hata katika vipindi ambapo viongozi watakapobadilishwa na kuletwa wengine.

Amesema Ofisi ya Rais TAMISEMI itaweka mkazo wa kudhibiti matumizi mbalimbali fedha za miradi ya maendeleo na matumizi mengineyo katika Halmashauri ili kuhakikisha taratibu za kifedha zinazingatiwa.

Aidha, Waziri Kairuki amesema atasimamia Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa kuziba mianya ya upotevu wa fedha za umma kwa kujiridhisha kuwa matumizi yanayofanyika ni yale yanayohitajika.

Katika ukusanyaji na ukadiriaji mapato, Waziri Kairuki amesema kuna baadhi ya Halmashauri hukadiria viwango vya chini ili kwenye makusanyo waonekane wamevuka lengo, hivyo katika mwaka wa fedha ujao watapitia kila Halmashauri kujiridhisha vyanzo vya mapato na makadirio yao.

Amesema atahakikisha katika Mamlaka za Serikali za Mitaa wanaboresha mazingira ya biashara na uwekezaji kwa kubuni vyanzo vipya vya mapato ili kukuza mapato katika Halmshauri.

Vile Vile, Waziri Kairuki amesema TAMISEMI itaweka makazo katika usimamizi wa utoaji wa huduma mbalimbali kama afyamsingi, elimu na uboreshaji wa miundombinu barabara kupitia TARURA ili kuboresha maisha ya Watanzania.

Pamoja na mambo Mengine, Wizara itawajengea uwezo wa watumishi ili watekeleze vyema majukumu yao katika Mamlaka za Serikali za Mitaa ikiwa ni pamoja na kuendeleza kazi ambazo watangulizi walifanya katika Ofisi ya Rais -TAMISEMI.

By Jamhuri