Mwandishi Wetu, JamhuriMedia

Serikali imesema hadi kufikia Desemba 2023 vijiji vyote 758 mkoani Mtwara vitakuwa vimepata umeme.

Akizungumza mkoani Mtwara, tarehe 21 Septemba, 2023, Naibu Waziri wa Nishati Judith Kapinga amesema katika vijiji hivyo vingi vilikuwa havina umeme, hivyo watapeleka umeme katika maeneo hayo yote.

Amesema lengo la ziara yake hiyo mkoani humo ni kujionea hali ya uzalishaji umeme, kutembelea miradi inayotekelezwa kupitia mashirika yaliyo chini ya Wizara ya Nishati ikiwemo Shirika la Usambazaji Umeme nchini (Tanesco)  na Wakala wa  Huduma za Umeme Vijijini (REA), Awamu ya Tatu mzunguko wa pili.

Naibu Waziri wa Nishati Judith Kapinga alipomtembelea Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, ofisini kwake, tarehe 21 Septemba 2023.

“Nimepata fursa ya kutembelea mitambo inayozalisha umeme katika mkoa huu, hali ya uzalishaji umeme imekuwa hivj, kwa sababu kuna matengenezo yanaendelea na tunategemea baada  ya kukamilika hali ya uzalishaji umeme itaenda kuongezeka,” amesema Naibu Waziri Kapinga..

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali Ahmed Abbas amesema mkoa huo una jenerata 13 ambazo kama zingekuwa zinafanya kazi vizuri zingekuwa na uwezo wa kuzalisha megawati 26.5 na mahitaji hayazidi megawati 22.5, ambazo zilifikiwa kwa ukubwa huo mwaka 2021.

Amesema kutokana na uchakavu mkubwa wa mashine hizo, zimekuwa zikitoka kwenye mfumo, hivyo kupungua uwezo wa uzalishaji hali iliyosababisha kuwepo kwa malalamiko ya wananchi kuhusu upatikanaji wa umeme.

Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Innocent Luoga, amesema pamoja na hali ya umeme kutokuwa mzuri mkoani humo, lakini jitihada zinafanyika za kuboresha hali ya umeme katika mkoa huo.

Amesema mahitaji ya hali ya umeme yamekuwa yakiongezeka na mitambo ya awali katika mkoa huo ilifungwa 2006 yenye uwezo wa megawati 18, mashine 9 ambazo kila moja ilikuwa na megawati 2, huku mahitaji ya mkoa wa Mtwara na Lindi zilikuwa megawati 16.

Amesema kutokana na mahitaji yaliyopo kwa sasa, wameongeza hali ya upatikanaji huduma kwa kufunga mitambo mipya ya megawati 8.6 ili kukidhi mahitaji hayo.

Habari katika picha, wakati Naibu Waziri wa Nishati Judith Kapinga alipomtembelea Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, ofisini kwake, tarehe 21 Septemba 2023 Mtwara.

By Jamhuri