Na Byarugaba Innocent, JamhuriMedia, Kibaha

Jumla ya Shilingi 1,261,950,000.00 zinatarajia kukamilisha ujenzi wa vyumba vya madarasa 22,Ofisi 1 ya walimu,mabweni 3 na nyumba 4 za walimu zenye uwezo wa kuweka familia 8 zinazoendelea kujengwa kwenye Halmashauri ya Mji Kibaha ili kuboresha mazingira kwa walimu na wanafunzi na kufanikisha ufundishaji na ujifunzaji wa masomo

Aidha,vyumba hivyo vya madarasa ni pamoja na umaliziaji wa maboma yaliyoanza kujengwa kwa nguvu za wananchi kwa lengo la kuwanusuru wanafunzi kukaa chini na Sasa Serikali inakuja kuwaunga Mkono

Mkuu wa Divisheni ya Mipango na uratibu wa Halmashauri ya Mji Kibaha Wambura Yamo amesema Serikali ya Awamu ya Sita inatambua kuwa Taifa lolote lenye Maendeleo huwekeza kwenye sekta ya Elimu ambavyo Dkt.Samia Suluhu Hassan anawekeza kwa kuimarisha miundombinu,kutoa Elimu bure,kuboresha maslahi ya Walimu sambamba na kujenga nyumba za walimu ili kuwaongezea morali ya ufundishaji.

Mkuu wa Divisheni ya Elimu Sekondari,Rosemary Msasi ameeleza kuwa tangu Serikali ianze kutoe Elimu bila malipo wazazi na walezi wamehamasika kuwaandikisha wanafunzi shuleni hali inayofanya kuongezeka kwa uhitaji wa madarasa na Madawati ingawa Serikali imekuwa ikiyaongeza mara zote ili kuwafanya wanafunzi kufurahia masomo yao

Protasi Dibogo ni Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Kibaha ameahidi kuwa kazi yake na wataalam ni kusimamia ujenzi na kuhakikisha unakamilika kwa wakati,huku ubora ukizingatiwa ili thamani ya fedha isadifu miradi inayotekelezwa.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Kibaha Mhe.Mussa Ndomba amemshukuru Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan,Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa niaba ya wananchi na kuahidi kuwa Waheshimiwa Madiwani wote wataendelea kuisimamia Halmashauri ili miundombinu yote inayojengwa ifae Sasa na Miaka ijayo kulingana na ubora wake.

By Jamhuri