Na Mwandishi Wetu,JamhuriMedia,Dar

Wazazi wameshauriwa kuzingatia malezi na maadili kwa watoto wao ili kupunguza idadi ya watoto wanaojiingiza katika makundi yasiyofaa na kusababisha kufanya matendo yanayoishangaza jamii.

Ushauri huo umetolewa leo Oktoba 12, 2022 na Amiri wa Baraza Kuu la Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh Mussa Yusuph Kundecha, wakati akitangaza matokeo ya mtihani wa darasa la saba wa elimu ya dini ya kiislamu uliofanyika Septemba 14, mwaka huu iliyo chini ya taasisi ya Taasisi ya Islamic Education Panel.

Amesema kuwa kutokana na baadhi ya wazazi hushindwa kuwasimamia ama kuwalea watoto wao katika maadili mema kumechangia kujiingiza katika matumizi ya dawa za kulevya,ushoga,wizi,ubakaji.

“Kumekuwa na matukio mengi ya ajabu na ya kusikitisha sana na hii yote inatokana na wazazi kushindwa kuwaleta katika maadili mema watoto wao na mwisho hujiingiza katika matendo mabaya hivyo kupitia elimu ya dini itasaidia kupunguza matukio hayo,” amesema.

Amiri wa Baraza Kuu la Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania,Sheikh Mussa Yusuph Kundecha (katikati),akitangaza matokeo ya mtihani wa darasa la saba wa elimu ya dini ya kiislamu uliofanyika Septemba 14,mwaka huu.Kulia ni mwenyekiti wa taasisi ya Taasisi ya Islamic Education Panel.Mpigapicha Wetu

Kundecha amesema kuwa, katika mtihani huo jumla ya shule 3710 katika mikoa 25 na Halmashauri 151 zilishiriki kufanya mtihani ambapo jumla ya watahiniwa waliosajiliwa walikuwa 163,143 na waliofanya mtihani ni 142,522 sawa na asilimia 87.36 na ambao hawakufanya kutokana na sababu mbalimbali ni 20.621.

“Mwaka 2021 mikoa 30 ilishiriki ina idadi ya shule zilikuwa 3667 na idadi ya watahiniwa ilikuwa 126,088 na mwaka huu wa 2022 mikoa 25 imeshirikia na idadi ya shule zilikuwa 3710 na watahiniwa 142,522 ambapo kupungua kwa idadi ya mikoa imetokana na mikoa ya Zanzibar kutoshiriki katika mitihani wa mwaka huu kutokana na sababu za kisera.

‘Idadi ya watahiniwa waliofanya mitihani imeongezeka kwa watahiniwa 16,434 sawa na asilimia 13.03 kutoka watahiniwa 126,0888 mwaka 2021 hadi watahiniwa 142,5222 mwaka 2022,” amesema.

Mwenyekiti wa Taasisi ya Islamic Education Panel Mohamed Kassim amesema kuwa shule 10 bora zenye watahiniwa 20 au zaidi ni Mumtaaz (Mwanza),Istiqaama (Tabora),Rahma (Dodoma),Algebra Islamic (Dar),Dumila (Morogoro,Islamia (Mwanza),Hedaru (Kilimanjaro),Daarul Arqam (Dar),Mbagala Islamic (Dar),Maarifa Islamic (Dar).

Pia alizitaja halmashauri 10 bora ni ambapo ikiongozwa na Hamashauri ya Wilaya ya Songea (Ruvuma), Mji wa Newala (Mtwara),Ngorogoro (Arusha),Ukerewe (Mwanza),Kalambo (Rukwa),Newala (Mtwara),Tunduma (Songwe),Mafia (Pwani), Mkuranga (Pwani) na Mji Nzega (Tabora).

By Jamhuri