Kwa nini mazishi ya Malkia Elizabeth II ni mazishi ya karne

Mabilioni ya watu duniani wanatarajia kufuatilia maziko ya Malkia Elizaberth II le huku kukiwa na wageni 2000,viongozi 500 wa kigeni na wahudumu 4,000.

Mazishi ya kitaifa ya Malkia Elizabeth II litakuwa tukio kubwa zaidi na la kipekee katika Karne ya 21 na tukio lisilo na kifani.

Ukiacha taratibu za mazishi na maombolezo,saa 48 zijazo pia zitashuhudia mkusanyiko mkubwa zaidi wa viongozi wa ulimwengu na wanasiasa pengine kuwahi kutokea.

Wafalme, wakuu, marais na mawaziri wakuu wako jijini London kwa mazishi huko Westminster Abbey.

Rais wa Marekani Joe Biden na mkewe Jill Biden wakiondoka Marekani jana kuelekea Uinhereza kuhudhuria maziko ya malkia

Bila shaka, matukio yatakayokuwepo ni ukumbusho muhimu sana wa kifo cha Malkia heshima ya kimataifa kwa mwanamke ambaye alikuwa mmoja wa viongozi wa ulimwengu wanaotambulika kwa muda mrefu.

Mwanadiplomasia mmoja mkuu aliiambia BBC: “Kila mtu anataka kuja kwenye mazishi ya Malkia kwa sababu yeye ni mmoja wa familia. Kuna hisia ya kuwa haya ni mazishi ya familia.

Mwanadiplomasia mwingine alisema “Haya ni mazishi ya karne. Kila kiongozi wa dunia atataka kushuhudia na kuonekana. Wale ambao hawatakuwa hapa na hawataonekana watapoteza picha kubwa zaidi na kumbukumbu muhimu ya nyakati zetu.”

Lakini pia mazishi ya malkia ni nafasi kwa ulimwengu, na viongozi wenyewe, kuonana kwa karibu.

Huenda ikawa kwenye basi kuelekea Westminster Jumatatu asubuhi, (ndiyo, mawaziri wakuu na marais wanapanda basi) au inaweza kuwa katika umati wa mapokezi ya Mfalme siku ya Jumapili, Inaweza hata kuwa baada ya muda wa kufunga maziko yenyewe.

Bila kujali tukio lolote, wanasiasa na wanadiplomasia mara nyingi hutafuta wakati wa fursa – kwa neno la utulivu, unaweza kusema uhusiano mpya wa binafsi, na nafasi ya kujadili masuala muhimu.

Orodha ya wageni yenyewe ni kielelezo cha siasa na mamlaka kwa mwaka wa 2022. Ni idadi ndogo tu ya nchi ambazo zimetengwa kabisa Urusi na Belarusi hazikualikwa kwa sababu ya vita vya Ukraine. Nyingine Syria, Myanmar, Afghanistan na Venezuela wameachwa pia.

Ukiacha matukio na mambo mengine mengi, hata mpango wa ukaaji kwa viongozi na watu wengine mashuhuri unaonesha ukubwa na umuhimu wa tukio lenyewe. Balozi mmoja aliiambia BBC, matukio “hayatoi nafasi nyingi kwa shughuli za kidiplomasia”. Viongozi wa ulimwengu wanaoingia ndani wako hapa kwanza kabisa kuonyesha heshima zao.

Kipindi kirefu cha utawala wa Malkia na umashuhuri wa maziko yake kidiplomasia ni jambo la kipekee. Ni hafla isiyo na mfano kwa ulimwengu wa sasa. Alihusika katika upangaji wake wa kina na labda hakuna mtu aliyeelewa nguvu na ukubwa wa tukio lililopangwa kwa uangalifu kama marehemu Malkia mwenyewe.