Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia

KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Daniel Godfrey Chongolo amesimikwa uchifu na wazee wa kabila la Wafipa mkoani Rukwa na kukabidhiwa mkuki na upinde na kuvalishwa mgolole, huku wakiomba wajengewe makumbusho ya labila la Wafipa.

Tukio hilo liliongozwa na Chifu wa Kabila la Wafipa, Chifu Malema Mtuka Sinyangwe, ambapo mapokezi ya Katibu Mkuu Chongolo yalifanyika Wilaya ya Nkasi baada ya kuingia Mkoa wa Rukwa akitokea Katavi, akiendelea na ziara ya kukagua utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2020/25, kusikiliza kero za wananchi na kuzitafutia ufumbuzi na kuhamasisha uhai wa CCM.

Chongolo alipokelewa eneo la Palamawe wilayani Nkasi mkoani Rukwa Jumapili Oktoba 8, 2023 na atakuwa katika mkoa huo kwa ziara ya siku tano.

“Ardhi hii ya Nkasi ikumbukwe kwamba harakati za kuutafuta ukumbozi wa nchi yetu, Wapigania uhuru walishirikisha sana wazee wetu waliotutangualia,” amesema Chifu Malema wakati akimsimika uchifu dugu Chongolo.

Aidha amesema fimbo ya kwanza katika taifa letu ilitoka ufipa kwa heshima ya baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere,na leo Serikali ya CCM imewapa heshima kubwa Wanarukwa kwa kumpeleka Mwana wa Baba wa Taifa Charles Makongoro Nyerere.

Baada ya kumsimika Katibu Mkuu wa CCM Daniel Chongolo kuwa Chifu wa Wafipa,Chifu Malema alitumia nafasi hiyo kuiomba Serikali kujenga makumbusho ya kuhufadhi Kumbukumbu za mila za Kifipa ili zisipotee kutokana na Utandawazi.