KATAVI

Na Walter Mguluchuma

Chama cha NCCR-Mageuzi mkoani hapa kimeunga mkono maazimio ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya chama hicho kumsimamisha uenyekiti James Mbatia na makamu wake, Angelina Mtahiwa.

Akitoa tamko la chama la mkoa, Kamishna wa NCCR Mkoa wa Katavi, Rajabu Makana, amelaani kundi linalomuunga mkono Mbatia lililojaribu kuwashawishi viongozi wa mikoa mbalimbali kupinga uamuzi uliotolewa na Halmashauri Kuu.

Akizungumza baada ya kikao cha Halmashauri Kuu ya NCCR Mkoa wa Katavi kilichohudhuriwa na viongozi wa majimbo matano mkoani hapa, Makana amesema Mbatia, aliyesimamishwa uongozi Mei 21, mwaka huu, amekuwa akituhumiwa kutumia vibaya mali za chama. 

“Mbali na tuhuma nyingine, pia amekuwa akishindwa kufanya kazi na viongozi wenzake na wamesimamishwa mpaka Mkutano Mkuu utakaposikiliza utetezi wao,” amesema.

Amesema kuna watu wanazunguka mikoani wakiwafuata wajumbe walioshiriki kupitisha uamuzi ngazi ya taifa ili wasaini nyaraka za kukana ushiriki wao.

“Kitendo hiki si sahihi. Kama viongozi hawa ni wasafi, wasubiri Mkutano Mkuu! Kuanza kushawishi wajumbe ni kuongeza makosa na kudharau vikao halali vilivyotoa uamuzi,” amesema.

Mwenyekiti wa NCCR Jimbo la Mpanda Mjini, Abdul Sigela, amesema akiwa kiongozi wa chama wa muda mrefu, anaunga mkono uamuzi wa Halmashauri Kuu ya Taifa, akiomba Mkutano Mkuu uitishwe haraka kumuidhinisha mwenyekiti mpya.

“Iwe hivyo ili kutoa nafasi kwa chama kuendelea kufanya kazi na kujiandaa kwa uchaguzi ujao wa Serikali za Mitaa na Uchuguzi Mkuu wa 2025,” amesema Sigela.

Kauli hiyo inaungwa mkono na Mwenyekiti wa chama hicho Wilaya ya Tanganyika, Muliton Mvilabo, akiwapongeza wajumbe walioshiriki kumwondoa Mbatia madarakani.

By Jamhuri