Naibu Waziri wa Nishati, Wakili Stephen Byabato, amesema kuwa utekelezaji wa mradi wa umeme wa Julius Nyerere (JNHPP) utakaozalisha umeme wa kiasi cha megawati 2,115 umefikia asilimia 80.2.

Naibu Waziri Byabato ameyasema hayo Januari 17, 2023, wakati Wizara ya Nishati ikitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi huo kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini jijini Dodoma.

“Kwa sasa utekelezaji wa mradi unaenda kwa kasi ambapo hadi kufikia tarehe 31 Desemba, 2022 umefikia asilimia 80.22, aidha mnamo tarehe 22 Desemba, 2022 zoezi la kuanza kujaza maji katika bwawa la JNHPP lilifanyika kwa kufunga mageti ya njia ya mchepusho,” amesema Byabato.

Naibu Waziri wa Nishati, Wakili Stephen Byabato (kushoto) akizungumza wakati Wizara ya Nishati ilipotoa taarifa ya utekelezaji wa mradi wa umeme wa Julius Nyerere (JNHPP)  kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini jijini Dodoma. Kushoto kwake Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Styden Rwebangila.

Kuhusu kazi ya ujazaji maji katika Bwawa la JNHPP amesema kuwa, hadi kufikia tarehe 16 Januari, 2023 kimo cha maji cha Bwawa kilifikia mita 112.48 kutoka usawa wa bahari kutokea kimo cha mita 74 tarehe 22 Desemba 2022.

Naibu Waziri ameongeza kuwa, utekelezaji wa mradi wa JNHPP unaenda sanjari na utekelezaji wa mradi wa njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kV 400 kutoka eneo la mradi hadi Chalinze mkoani Pwani na ujenzi wa kituo cha kupoza umeme cha Chalinze ambapo kwa ujumla miradi hiyo inaendelea kutekelezwa kwa kasi.

Kuhusu malipo kwa mkandarasi wa mradi huo amesema kuwa, tayari Serikali imeshalipa asilimia 74.7 ya malipo hayo ambapo gharama za mradi huo ni shilingi Trilioni 6.5.

Naibu Waziri wa Nishati, Wakili Stephen Byabato (mbele, kushoto) akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi wa umeme wa Julius Nyerere (JNHPP)  kwa Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini jijini Dodoma. Kushoto kwake Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Styden Rwebangila.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Dunstan Kitandula amepongeza Serikali kwa utekelezaji wa mradi huo ikiwemo hatua ya kuanza kujaza maji kwenye bwawa hilo. Aidha amesisitiza mradi huo kuendelea kutekelezwa kwa kasi ili asilimia za utekelezaji zilizobaki zikamilike kwa wakati.

Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati, Mhandisi Styden Rwebangila pamoja na watendaji wengine kutoka Wizara ya Nishati na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO).

By Jamhuri