Wakati mbio za NMB Marathon zikitarajiwa kutimua vumbi Septemba 24 mwaka huu, klabu ya NMB Jogging yenyewe jana Jumatatu ilianza kujifua mapema kwa ajili ya kujiweka tayari kushiriki mbio hizo.

Jogging hiyo ilianza kujiandaa na mbio hizo kushirikiana klabu ya EFM Jogging ambapo walianza maandalizi hayo kwa kukimbia mbio za kilomita nane. Mbio hizo zilianzia kwenye Ofisi za NMB, Posta jijini Dar.

Mbio hizo za NMB Marathon ambazo huu ni msimu wake wa pili zinatarajiwa kurindima katika Viwanja vya Leaders, Dar ambapo mgeni wake rasmi anatarajiwa kuwa Waziri Mkuu, Mhe. Kassim Majaliwa.

Mbio hizo zenye kauli mbiu ya Mwendo wa Upendo zinafanyika maalum kwa ajili ya kuchangisha fedha kusaidia matibabu ya akina mama wenye matatizo ya Fistula.

Meneja wa NMB Jogging, Stella Motto amesema wana siku chache kabla ya kufikia Septemba 24 ambapo NMB Marathon itafanyika, hivyo wameona wapashe misuli ili wawe sawa na kuwakumbusha wadau kujisajili na mbio hizo zenye lengo kuu la kukusanya fedha kwa ajili ya kina mama wenye matatizo ya fistula.

Kwa upande wake mwakilishi wa EFM, Tunu Hassan alisema “Hii siyo mara ya kwanza kwa NMB kurudisha kwa jamii, hivyo nasi tumeona tuungane nao kwa ajili ya jambo hilo.

Jisajili na NMB Marathon kupitia https://marathon.nmbbank.co.tz/ au sogea Mlimani City kila Jumasosi na Jumapili kuanzia saa 3 asubuhi mpaka 12 jioni. Pia, Mtana Bar(Oysterbay) na Juliana Pub( Mbezi Beach) Ijumaa, jumamosi na jumapili kuanzia saa 6:30 mchana mpaka saa 4 usiku.

By Jamhuri