JAMHURI MEDIA

Tunaanzia wanapoishia wengine

Latest Posts

Anahitajika Sokoine mwingine 2015

Mengi mazuri yanayomhusu Waziri Mkuu wa zamani wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Edward Moringe Sokoine, yamesemwa na yanaendelea kusemwa.

Kwa Mtanzania yeyote wa kweli, kamwe hatachoka kusikia mengi yaliyofanywa na Sokoine wakati wa uongozi wake.

Miaka 30 sasa tangu alipoaga dunia, shujaa huyu hajulikani kwa vijana wengi wa Tanzania. Safu hii ni fupi mno, kiasi kwamba haiwezi kumweleza japo kwa nukta mtu huyu hata akaeleweka kwa vijana wengi.

Itoshe tu kuwaasa vijana kuyasaka kwa udi na uvumba maandiko yanayomhusu shujaa huyu wa Tanzania, ambaye mfano wake kwenye nafasi ya Waziri Mkuu, haujapatikana.

Licha ya wengi kumzungumza Sokoine, hiyo haitoshi kutufanya nasi tusiweke neno wakati huu wa kumkumbuka.

Moringe alikuwa kipenzi cha Watanzania wengi, hasa makabwela. Alipendwa na watu wa jinsi, hali na rika zote. Hakuwa na makuu. Alikuwa mcha Mungu wa kweli. Hakuwa kiongozi wa kupayuka-payuka, bali alikuwa mpole, msikivu na mwenye kusimama katika ukweli na haki. Uwajibikaji na uadilifu ndiyo uliokuwa msingi mkuu wa Sokoine.

KAGAME NI MTIHANI Viongozi Maziwa Makuu waufanye kwa Uangalifu

Ni wazi kwamba nafasi inayoshikiliwa na Uganda na Rwanda katika roho ya uchumi wa Marekani na Uingereza ni kubwa kuliko nchi yoyote ile katika eneo la Maziwa Makuu kwa sasa.

Hakika Marekani na Uingereza wamelipa gharama kubwa kutengeneza miundo ya kiserikali, nguvu za kijeshi na saikolojia za kisiasa zinazoongoza nchi hizo miaka ya karibuni.

Watu walijiuliza maswali mengi kunako miaka ya tisini juu ya nguvu za Museveni na baadaye kasi ya RPF kuitwaa Rwanda, nchi ambayo ilikuwa imeanza kuimarika kama zilivyokuwa nchi nyingine barani Afrika. Hasa nchi ambazo zilikuwa zimeishi kwa amani toka uhuru mpaka miaka hiyo.

Mwanzoni mwa miaka ya tisini Rwanda ilikuwa na fedha yenye thamani kubwa. Ilikuwa pia na msaada mkubwa wa kijeshi kutoka Ufaransa. Raia wake walikuwa na kipato kizuri cha kutosha. Ilikuwa thabiti.

Matatizo yaliyokuwapo Rwanda miaka ya tisini yaliakisi matatizo yaliyokuwapo kwingineko barani Afrika kama vile vita za wenyewe kwa wenyewe, uongozi mbovu na uamuzi usiyo na tija, ufisadi wa wachache, upendeleo wa kikabila (Wahutu), undugu (nepotism) na zaidi suala la wakimbizi.

Wakimbizi wa Rwanda miaka ya ‘tisini mwanzoni’ walikuwa ni Watutsi waliokuwa wameikimbia nchi baada ya mapinduzi mwaka 1959 yaliyoiondoa dola ya mfalume Kigeri V muda mfupi kabla ya uhuru. Rwanda haikutofautiana na nchi nyingine nyingi barani Afrika.

Ukiilinganisha Rwanda ya sasa ya Kagame ambayo wapinzani wake wanaviziwa na kuuawa hata wakiwa nje ya nchi! Rwanda ambayo wakati wa uchaguzi raia wanapotea kimya kimya na baadhi kuokotwa wakiwa mizoga!

Hotuba ya Lissu iliyosababisha TBC1 ‘izimwe’

Aprili 12, mwaka huu, Mjumbe wa Bunge Maalum la Katiba, Tundu Lissu aliwasilisha maoni ya Wajumbe walio wachache katika Kamati Namba Nne kuhusu sura ya kwanza nay a sura ya sita ya Rasimu ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Wakati akiwasilisha, Televisheni ya Taifa (TBC1) ilikata matangazo yake katika kile kilichotafsiriwa na wengi kuwa ni kuuepusha umma kupata maoni ‘makali’ yaliyomo kwenye hotuba ya Lissu. Kwa kuzingatia haki ya wananchi ya kupata habari, JAMHURI inawaletea hotuba hiyo neno kwa neno. Endelea

UTANGULIZI

Mheshimiwa Mwenyekiti,

Sura ya Kwanza na Sura ya Sita ya Rasimu ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (‘Rasimu’) ndizo msingi ambao Rasimu yote imejengwa juu yao. Wakati Sura ya Kwanza inagusa suala la muundo wa Muungano katika ibara moja tu kati ya ibara tisa, Sura yote ya Sita inahusu ‘Muundo wa Jamhuri ya Muungano.’ Suala la Muungano na hasa Muundo wake limetawala mjadala wa kisiasa na kikatiba wa Tanzania kwa zaidi ya miaka thelathini. Ndio maana katika waraka wake wa siri kwa Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi (‘CCM’), Idara ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa ya chama hicho imetamka kwamba “muundo wa Muungano ndiyo moyo wa Rasimu na ndiyo unaoamua ibara nyingine zikae vipi.”

Suala hili pia limetawala mchakato wa Katiba Mpya tangu ulipoanza miaka mitatu iliyopita. Kama alivyosema Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Joseph Sinde Warioba wakati wa kuwasilisha Ripoti ya Tume yake kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano na Rais wa Zanzibar tarehe 30 Disemba, 2013: “Moja ya mambo ambayo yamejadiliwa sana na kwa hisia kali tangu Rasimu ya awali ilipotolewa … ni Muungano wa Tanzania. Jambo kubwa limekuwa juu ya muundo wa Muungano.”

Umuhimu wa suala hili unathibitishwa pia na uamuzi wa Kamati ya Uongozi ya Bunge Maalum kuelekeza kwamba Kamati zake Namba Moja hadi Kumi na Mbili zianze kujadili Sura ya Kwanza na ya Sita ya Rasimu. Haya ni maoni ya wajumbe walio wachache wa Kamati Namba Nne juu ya Sura hizi mbili.

Kipande, Magesa wakoroga ICT bandari

 

Madeni KipandeMamlaka ya Bandari Tanzania imegeuzwa sehemu ya ulaji wa hali ya juu. Hata hivyo, kutokana na mtandao mpana wa kuchota fedha unaoanzia wizarani hadi bandarini, yeyote anayetaka kuonesha paka yuko wapi, basi anaishia ama kufukuzwa kazi kwa njia ya vitisho, au kufanyiwa ‘kitu mbaya’.

Mkurugenzi Mkuu, Madeni Kipande, anamkingia kifua Mkurugenzi wa ICT, Phares Magesa, ambao kwa pamoja wanatuhumiwa kuzamisha jahazi la bandari Tanzania.

Baada ya kuchapisha sehemu ya kwanza ya matukio yanayoendelea bandarini, wiki hii JAMHURI inakumegea sehemu tu kati ya madudu mengi yanayoendelea bandarini, ambayo kwa kila hali yanadhihirisha kuwa Mkurugenzi Mkuu, Madeni Kipande, ama hajui kitu kinachoitwa utawala wa sheria, au amedanganywa na watu wanaombeba pale Ikulu, hivyo amepoteza mwelekeo.

Ifuatayo ni sehemu ya barua ya ushauri wa kitaalamu, ambayo ilitolewa na aliyekuwa Mkurugenzi wa Bodi, Mei mwaka jana, akieleza hatari inayoinyemelea bandari kutokana na mfumo wa mawasiliano (Information and Communication Technology – ICT) kuchezewa katika Bandari ya Dar es Salaam na hivyo kupoteza mapato, imani ya wateja na kuhatarisha mizigo inayopitia bandarini.

Kwa mshango wa wengi, Dk. Jabir Bakari aliyeandika barua hii na kutoa ushauri, kwa mizengwe tu kama alivyosema Kipande kwenye kikao kati ya Wakurugenzi wa Bodi na Dk. Mwakyembe, Agosti mwaka jana huko Dodoma, kuwa “yeye ni mteule wa Rais na hivyo wakurugenzi hawambabaishi”, Kipande alifanya mbinu Dk. Jabir akafukuzwa katika Bodi ya Wakurugenzi wa Bandari kwa kutoa ushauri huu. Ifuatayo ni tafsiri isiyo rasmi ya barua hiyo. Endelea…

Nyalandu aanza kuliliza Taifa

*Marekani yapiga marufuku nyara kutoka Tanzania Uamuzi tata na wa kijazba wa Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, umeanza kuleta athari kwa tasnia ya uwindaji wa kitalii nchini. Marekani imepiga marufuku nyara zinazotokana na ndovu kutoka Tanzania kuingizwa nchini…

Wakubwa wanavyotafuna Bandari

*Waanzisha EPA mpya, Bandari waitengea CCM bilioni 10
*Kinana aukana mradi, walipanga kujenga yadi ya malori
*Dk. Mwakyembe ampa onyo Kipande, agoma kuhojiwa
*Ikulu yakana kumlinda, wakili adai milioni 205/- kwa siku
*Mkurugenzi anyanyasa wanawake, Bodi ‘imewapotezea’
*Wataalamu waacha kazi TPA, Magesa akiri hakuna ulinzi

Utaratibu wa baadhi ya wanasiasa kuchota mabilioni ya shilingi kutoka kwenye Hazina ya Taifa kwa ajili ya maandalizi ya Uchaguzi Mkuu umeendelea.
Wakati mwaka 2005 zilitumika kampuni kama Kagoda, Deep Green na nyingine kuchota mabilioni ya EPA, zamu hii Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) wameanzisha mradi kama huo kwa ajili ya mwaka 2015, ambapo wameitengea CCM Sh bilioni 10 kwa ajili ya mradi wa kuegesha magari.
Habari za uhakika kutoka ndani ya Bandari, ambazo gazeti JAMHURI limezithibitisha, bajeti ya Mamlaka ya Bandari inaonesha kuwa wajanja wametumia kampuni tanzu ya CCM (SUKITA) Sh bilioni 10 kama kianzio kwenye bajeti ya mwaka huu kwa ajili ya mradi wa kuegesha malori.
Mradi huu umeingizwa kiujanja kupitia Kampuni ya Lori Parking Yard kwenye Bonde la Msimbazi, eneo la Tabata Matumbi yaliko majengo ya SUKITA. JAMHURI imeshuhudia pilikapilika za ujenzi katika eneo hilo.
“Huwezi kuamini, huu ni mradi hewa. Wanatafuta fedha za Uchaguzi Mkuu mwaka 2015. Kwenye bajeti ya 2014/2015 wanasema kiasi cha Sh bilioni 10 kilichotengwa ni cha kuanzia. Mwakani kitatengwa kiasi kikubwa zaidi. Lakini ukiangalia uhalisia, hata kama kweli wangekuwa wanajenga maegesho ya malori, eneo hili haliruhusu uwepo wa maegesho haya.
“Pale Tabata ni katikati ya jiji kwa sasa, tuna msongamano mkubwa wa magari kuelekea kwenye makutano ya Ubungo, leo unasema unaweka yadi ya kuegesha malori Tabata! Utatengeneza msongamano wa kiasi gani? Kama ni yadi ya malori ilipaswa kujengwa hata nje ya Kibaha kuelekea karibu na Mlandizi, ila si katikati ya jiji. Lakini tunaojua, tunasema wajinga ndiyo waliwao. Ni mradi wa uchaguzi,” kilisema chanzo chetu.