Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Samia Suluhu Hassan ameteuliwa rasmi kuwa Mjumbe wa Bodi ya Ushauri ya Kituo cha Dunia cha Uhimilivu wa Mabadiliko ya Tabianchi (Advisory Board of the Global Centre on Adaptation – GCA).

Taarifa ya uteuzi huo iliwasilishwa na Ban Ki-moon, Mwenyekiti wa Bodi ya GCA na Katibu Mkuu Mstaafu wa Umoja wa Mataifa alipokutana na Rais pembezoni mwa Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Afrika kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi uliofanyika Nairobi, Kenya.

Heshima hii ni utambuzi wa uongozi mahiri wa Rais Samia katika jitihada za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi Afrika na duniani kote ambapo Tanzania ni kinara kwenye utekelezaji wa miradi mbalimbali barani Afrika.

Wajumbe wengine wa Bodi hiyo ni Rais wa Jamhuri ya Senegal Mhe. Macky Sall, Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika Mhe. Moussa Faki Mahamat, Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Mhe. Akinumwi Adesina na Mkurugenzi Mwendeshaji wa Mfuko wa Fedha wa Kimataifa (IMF) Mhe. Kristalina Georgieva.

GCA ni taasisi kubwa duniani inayosimamia masuala ya uhimilivu wa mabadiliko ya tabianchi, ambapo hadi sasa imeweza kufanikisha upatikanaji zaidi ya Dola za Marekani bilioni 50. Tanzania ni miongoni mwa nchi za kwanza zitakazonufaika na fedha hizo katika kipindi cha miaka mitatu ijayo.

Zuhura Yunus
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu

By Jamhuri