Na Dotto Kwilasa, JamhuriMedia, Dodoma.

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.Samia Suluhu Hassan ameshuhudia hafla ya utiaji saini mikataba mitatu ya makubaliano yenye thamani ya Euro 179.35 milioni sawa na shilingi za kitanzania bilioni 455.09 msaada uliotolewa na umoja wa Ulaya(EU).

Aidha hafla hiyo imeambatana na kupokea msaada wa bajeti ya Serikali kiasi cha Euro 46.11 milioni sawa na shilingi bilioni 117.036 za Tanzania kwa mwaka wa fedha 2022/2023 kutoka Umoja huo.

Mikataba hiyo ni pamoja na uimarishaji wa uchumi wa Blue wenye thamani ya Euro 110 ambao utaelekezwa kwenye maeneo ya pwani na Zanzibar, mkataba wa kuimarisha mifumo ya usimamizi wa fedha Serikalini na sekta binafsi wenye thamani ya Euro 50 milioni na mkataba wa mradi wa kuimarisha mikopo ya masomo wenye thamani ya Euro 6 milioni.

Akizungumza kwenye hafla hiyo leo Julai 4,2023 Jijini Dodoma,Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ameihakikishia jumuiya hiyo (EU) kuwa fedha hizo zitaelekezwa kwa usahihi kwenye matumizi yaliyokusudiwa.

Amesema hatua hiyo itaendeleza mahusiano mazuri kwa nchi ya Tanzania na umoja huo na kuiwezesha Tanzania kufanikisha malengo ya maendeleo endelevu.

Rais Samia pia ametumia nafasi hiyo kuiomba EU kuona namna ya kuwasaidia wakulima kupitia benki ya kilimo na mpango wa BBT kwa kutoa mikopo yenye unafuu hali itakayosaidia kuchochea maendeleo ya kilimo nchini.

Naye Balozi wa EU Manfredo Fanti ameeleza kuwa umoja huo utaendelea kuisaidia Tanzania na kwamba jambo hilo linawapa fahari kwa kuwa wanaamini Fedha walizotoa zitaenda kuwasaidia watanzania na kuwapa unafuu.

Amesema kupitia mikataba hiyo mitatu uchumi wa wananchi utaimarika na kuimarisha usimamizi wa fedha.

Kwa upande wa Waziri wa fedha na mipango Dk.Mwigulu Nchemba aleeza kuwa kupitia mikaba hiyo ni wazi kuwa utekelezaji wa mifumo ya fedha za umma utaenda kuboreshwa na kuondokana na upotevu wa fedha usio na tija.

Akizungumzia Bajeti ya Serikali amesema kiasi cha Euro 46.11 milioni ambazo ni sawa na shilingi bilioni 117.036 za Tanzania kwa mwaka wa fedha 2022/2023 kutoka zitaelekezwa kuweka unafuu kwenye masuala mbalimbali ikiwemo umeme vijiji,maji naendeleo ya jamii.

By Jamhuri