Na Mwandishi Wetu,JamhuriMedia, Dodoma

Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu, amesema katika kukabiliana na changamoto ya sasa ya uhaba wa Watumishi, Serikali imetoa kibali cha kuajiri jumla ya Watumishi 13,187 katika Sekta ya Afya huku pia ikichukua hatua ya kutekeleza mwongozo wa ajira za mikataba ya muda mfupi kwa kutumia mapato ya ndani, ambapo jumla ya Wataalamu 4,838 waliajiriwa kwa utaratibu wa ajira za mikataba ya muda mfupi kwa kutumia mapato ya ndani.

Akiwasilisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha kwa Mwaka 2024/2025 Bungeni jijini Dodoma leo, Waziri Ummy amesema kati ya Watumishi hao walioajiriwa kwa ajira za mikataba, Watumishi 4,183 wameajiriwa kwenye Hospitali za Rufaa za Mikoa, Kana, Maalum na Hospitali ya Taifa Muhimbili na Watumishi 655 wameajiriwa ngazi ya afya ya msingi.

Waziri Ummy pia amesema hadi kufikia mwezi Machi 2024, Sekta ya Afya ilikuwa na jumla ya Watumishi wa Afya 126,925 ambao ni sawa na asilimia 57.9 ya Watumishi wote 219,061 wanaohitajika katika Sekta ya Afya kulingana na IKAMA ambapo kati yao, Watumishi 101,733 sawa na asilimia 80.2 wapo katika ngazi ya afya ya msingi na Watumishi 25,192 sawa na asilimia 19.8 wanafanya kazi katika ngazi ya Hospitali za Rufaa za Mikoa, Kanda, Maalum na Taifa.