Na Dotto Kwilasa, Jamhurimedia,Dodoma

SERIKALI ya Tanzania kwa kushirikiana na Korea imechukua hatua za kukabiliana na changamoto za ardhi kwa kuanzisha kituo cha Ubunifu na mafunzo ya teknolojia na taarifa za kijiografia (TNGC)hali itakayo boresha majukumu ya kupanga,kupima na kimilikisha Ardhi bila uwepo wa migogoro.

Kutokana na hatua hiyo Serikali imeitaka Wizara ya ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kushirikiana na Wizara na taasisi zote za serikali kuweka mfumo mmoja utakao wezesha kutoa taarifa za Kijiografia wakati wa kupima miji ili kumaliza migogoro ya Ardhi iliyopo.

Naibu Waziri Mkuu wa Tanzania Dk.Doto Biteko ameyasema hayo leo September 9,2023 jijini Dodoma kwenye Hafla ya ufunguzi wa kituo Cha Taifa cha ubunifu na mafunzo ya Teknolojia ya taarifa za Kijiografia akimuakilisha Waziri Mkuu Kasimu Majaliwa.

Amesema wizara ya ardhi ni wizara mama ambapo karibu kila wizara zimekuwa zikiigusa hivyo mashirikiano mazuri kwa wizara nyingine ndizo zitaweza kuandoa migogoro kwa kuhakikisha Maeneo yanapimwa na kurasimishwa kuepuka migogoro.

Amesema mara kwa mara kumekuwa na wimbi la kuondoa na kuhamisha malengo ya Wizara ya ardhi na kuitoa kwenye majukumu yake na kuonekana ni Wizara ya utatuzi wa migogoro jambo ambalo linakera na kuitaka Wizara hiyo kujikita kwenye majukumu yake mipango miji,mandeleo ya makazi na matumizi bora ya Ardhi …

” Kumekuwepo na wimbo la migogoro isiyoeleweka na mtatuzi wake ni wizara na iko wazi panapotokea migogoro kuna mtu katikati sasa niwaombe twendeni tukafanye kazi tuliosemea kwa weledi na tukifanya hivyo tutakuwa tumeondokanà na kero ya Ardhi,”amesisitiza.

Naye Waziri wa Ardhi,Nyumba na maendeleo ya makazi Jerry Silaa amesema Serikali ya Tanzania Kwa kushirikiana na Serikali ya Korea imechukua hatua za kukabiliana na changamoto za ardhi kwa kuanzisha kituo cha TNGC .

Amesema Wizara hiyo ina changamoto ya ukosefu wa teknolojia za kisasa katika upatikanaji wa taarifa za kijiografia na mifumo ya usimamizi wa ardhi na kupelekea kupungua kwa kasi ya upangaji , upimaji,uthamini na umilikishaji ardhi hivyo kituo hicho kinatarajiwa kumaliza kero zote.

“Serikali yetu imeweka historia leo ya kuweka alama mbili muhimu ambayo ni kuzindua kituo cha kitaifa Cha Ubunifu na mafunzo ya taarifa za kijiografia na kuwatunuku vyeti wahitimu 11 waliopata mafunzo ya kurusha ndege zisizo na rubani tatu ,ukusanyaji wa taarifa za kijiografia na uchakataji wa taarifa za kijiografia,”amesema.

Silaa ametumia nafasi hiyo kuwataka Viongozi wa TNGC kujipanga na kuwa na maono ya kukiendeleza kituo ili kiwe Taasisi pekee ya Ubunifu na usimamizi wa taarifa za kijiografia nchini na kwamba Wizara itaendelea kutoa ushauri na kukilea kituo hicho .

“Serikali itaendelea kukiwezesha kituo ili kifikie malengo yake na kusaidia kutatua changamoto ya wataalam wenye weledi na ujuzi wa teknolojia ya kisasa ya usimamizi taarifa za kijiografia,”amesisitiza

Kwa upande wake Balozi wa Korea Nchini Tanzania Kim Sun Pyo amesema kuzinduliwa kwa kituo hicho ni manufaa kwa wananchi wa Dodoma kwani wataweza kunufaika hasa Katika Suala zima la upimaji wa ardhi ambao Sasa unakwenda kufanyika kwa ubora na kwabai nafuu.

Ameeleza kuwa mbali na kituo hicho kuongeza ushirikiano baina ya Tanzania na Korea kina lengo la kujengea uwezo watumishi na wadau kukidhi mahitaji ya teknolojia ya kisasa ya usimamizi wa taarifa za kijiografia nchini kwa kutoa mafunzo yenye ujuzi maalum.

Amesema TNGC ni fursa ya kuanzishwa kwa miundombinu ya kitaifa ya taarifa za kijiografia nchini na kwamba itasaidia kusambaza na kubadilishana taarifa Kwa manufaa ya Watanzania.

By Jamhuri