Na Mwamvua Mwinyi, JamhuriMedia, Pwani

KATIBU Tawala Mkoani Pwani Rashidi Mchatta ,ametoa rai kwa wajasiriamali wadogo kuzingatia uzalishaji wa bidhaa kitaalam na zenye ubora ili kukuza biashara zao na kuinua uchumi wa mkoa huo.

Mchatta ameyasema hayo wakati akikabidhi vyeti vya kwa wajasiriamali wenye viwanda vidogo na vidogo kabisa wa mkoa huo ambao wametambuliwa na Shirika la Viwanda Vidogo Vidogo (SIDO) Mkoa wa Pwani.

Amesema kuwa wajasiamali hao wanapaswa kuzingatia ubora na viwango pia kushirikiana na taasisi zinazothibitisha viwango vya bidhaa ili ipate soko ndani na nje ya nchi.

Aidha ameipongeza SIDO kwa jitihada za kuwawezesha wajasiriamali ambapo Mkoa huo una jumla ya viwanda 1,533 vikubwa 122 vya kati 120 vidogo 274 na vidogo sana 1,117.

Naye Meneja wa SIDO Mkoa wa Pwani Beata Minga amesema ,mkoa unatambua jitihada za wajasiriamali ambao wameanzisha viwanda ambavyo vitaongeza ajira na kuongeza pato la mwananchi mkoa na Taifa.

Minga amefafanua, vyeti hivyo vya kuwatambua vitawasaidia pale wanapohitaji kutambuliwa na taasisi nyingine ambazo ni za uwezeshaji .

Zoezi hilo litakuwa endelevu ambapo jumla ya wajasiriamali 65 wametambuliwa.

By Jamhuri