Katika muendelezo wa ziara za kushtukiza, Waziri wa Afya,Ummy Mwalimu leo amefanya ziara ya kushtukiza katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mwananyamala kukagua utoaji wa huduma, kusikiliza, kero, ushauri na maoni ya wananchi wanaopata huduma za matibabu katika Hospitali hiyo.

Aidha Waziri Ummy ametumia nafasi hiyo pia kutoa elimu ya Bima ya Afya na kuwaasa wananchi kujiunga na skimu mbalimbali za Bima ya Afya kabla ya kuugua ili kuwa na uhakika wa matibabu endapo wataugua.

Waziri Ummy amewataka watoa huduma katika Hospitali hiyo kuboresha zaidi ubora wa huduma na kuhakikisha wananchi wanahudumiwa vyema kulingana na sheria, kanuni, taratibu na maadili ya kitabibu na kuzingaia muda wa utoaji huduma hizo kwa wagonjwa kwa kutowaweka muda mrefu na vikwazo katika upatikanaji wa huduma.

Waziri Ummy Mwalimu amewapongeza watoa huduma kwa kuwa mstari wa mbele katika kuokoa maisha ya watu kupitia utoaji wa huduma bora za matibabu na kuwaasa waendelee kufanya kazi kwa juhudi na maarifa zaidi.

By Jamhuri