Zaidi ya mil.183/-kuhudumia Timu za Taifa

Na Shamimu Nyaki,JamhuriMedia, Dodoma

Naibu Waziri wa Utamaduni,Sanaa na Michezo Pauline Gekul, amesema kiasi cha shilingi Milioni 183.5 zimetengwa katika mwaka huu wa fedha 2022/23 kwa ajili ya kuhudumia timu za Taifa.

Gekul ameeleza hayo Bungeni jijini Dodoma leo Septemba 22, 2022 wakati akijibu swali la Janeth Elius Mahawanga (Viti Maalum) aliyeuliza ni lini Serikali itawekeza katika Sekta ya Michezo hasa kwenye timu za Wanawake, ili kuibua vipaji kwa watoto.

“Serikali imefanya uwekezaji mkubwa katika timu za Taifa za Wanawake ambapo kupitia uwekezaji huu, timu hizi zimeendelea kufanya vizuri katika ukanda wa CECAFA na COSAFA na pia umeiwezesha timu ya Serengeti Girls kufuzu Mashindano ya Kombe la Dunia nchini India” amesisitiza Mhe. Gekul

Aidha, akijibu swali la nyongeza la Mbunge huyo, kuhusu Serikali kukuza vipaji vinavyotokana na Mashindano ya UMITASHUMTA na UMISSETA, Naibu Waziri Gekul amesema, Wizara hiyo kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia pamoja na Ofisi ya Rais TAMISEMI zinashirikiana kuhakisha michezo hiyo inaendelea na inakuza na kutengeneza Wanamichezo wengi kwa ajili ya taifa na kutengeneza ajira.

Gekul,ametumia nafasi hiyo kumpongeza na kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Samia Suluhu Hassan kwa kurudisha michezo hiyo ambayo inaendelea kuzalisha wanamichezo wengi nchini.