Mwaka huu, Tanzania inaye Rais wa Awamu ya Tano, Dk. John Pombe Magufuli. Rais Magufuli, ameonyesha nia ya dhati ya kupambana na vitendo vya rushwa nchini, na hasa baada ya kuanzisha rasmi mchakato wa Mahakama ya Mafisadi kwa kuitengea bajeti katika mwaka huu wa fedha. Katika kuunga mkono juhudi zake, Gazeti la JAMHURI, linaloanzia wanapoishia wengine, limeamua kuchapisha Ripoti ya Rushwa ya Jaji Warioba aliyoitoa mwaka 1996.

Kwa hali ya kawaida, Ripoti hii bado iko sahihi kwa asilimia 100, na hivyo inahitaji kufanyiwa kazi. Ripoti hii katika baadhi ya maeneo inataja wala rushwa kwa majina na vyeo vyao. Ripoti hii iliyoandaliwa kwa umakini wa hali ya juu ikifanyiwa kazi, Tanzania yenye neema itawadia haraka. Isome…

 

SURA YA KWANZA

UTANGULIZI

1. Tarehe 17 Januari, 1996, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliteua Tume ya Kuchunguza Kero ya Rushwa nchini. Tume hii ina wajumbe wafuatao:  

1. Mh. J. S. Warioba – Mwenyekiti

2. Bw. I. M. Kaduma – Mjumbe

3. S.  Mworia – Mjumbe

4. Bw. L.T. Gama – Mjumbe

5. Bibi H. Kasungu – Mjumbe

6. Bw. Salim J. Othman – Mjumbe

7. Brig. H. I. Mbita – Mjumbe

8. Balozi F. Kazaura – Mjumbe

9. Bw. A. A. Muganda – Katibu

Ilipofika mwezi Machi, 1996, Balozi F. Kazaura aliteuliwa kuwa Katibu Mkuu Jumuiya ya Ushirikiano wa Nchi za Afrika Mashariki na Mheshimiwa Rais alimteua Bwana J. Sepeku kuchukua nafasi yake. Tume ilisaidiwa na Sekretarieti iliyoongozwa na Katibu.

 

2. Kulingana na barua ya Rais ya tarehe 17 Januari, 1996, Tume iliundwa chini ya Sheria ya Tume ya Uchunguzi sura ya 32, kifungu cha 2(1) na ilipewa hadidu za rejea zifuatazo:

(a)  Kutathmini sheria, kanuni na taratibu ili kubainisha mianya ya rushwa  kuhusu:-

(i) Ukadiriaji na ukusanyaji kodi

(ii) Utoaji leseni na vibali mbalimbali

(iii) Taratibu za ununuzi, hususani utoaji wa tenda

(iv) Taratibu za kudai na kutoa haki 

(v) Taratibu za kutoa huduma za jamii

(b) Kuchunguza ubora wa sheria, kanuni na taratibu zilizopo zinazosimamia mapambano dhidi ya rushwa na kupokea mapendekezo ya jinsi ya kuziboresha.

(c) Kuchunguza uwezo na uhusiano wa vyombo vinavyosimamia mapambano dhidi ya rushwa na kushauri jinsi ya kuviimarisha.

(d) Kubuni mikakati na mbinu mpya za kupambana na rushwa.

(e) Kuchunguza na kutoa ushauri kuhusu utekelezaji bora wa Sheria ya Maadili  ya Uongozi ya 1995, kwa lengo la kujenga imani ya wananchi katika uadilifu wa viongozi.

(f) Kupokea malalamiko, maoni na ushauri kutoka kwa wananchi kama mtu mmoja mmoja au kama vikundi au kama jumuiya.

(g) Kuwasilisha kwenye vyombo vinavyohusika malalamiko au taarifa kutoka kwa wananchi kuhusu vitendo vya rushwa ambavyo vinahitaji uchunguzi wa mara moja.

3. Tume ilitakiwa kufanya kazi katika muda usiozidi miezi tisa. Katika kipindi hicho Tume inaweza wakati wowote kukamilisha na kuwasilisha serikalini taarifa juu ya suala lolote inalolifanyia kazi ikiwa itaona linahitaji kuchukuliwa hatua mapema zaidi.

 

UTARATIBU WA KUFANYA KAZI

4. Tume ilifanya kikao chake cha kwanza tarehe 26 Januari, 1996 ambacho kiliandaa na kuweka mikakati ya utekelezaji wa kazi zake. Tume iliandaa taarifa kwa vyombo vya habari kueleza majukumu yake na kuwaomba wananchi kutoa maoni yao ama kwa maandishi au kufika kwenye Ofisi ya Tume. Pamoja na kupitia sheria mbalimbali zilizotajwa katika hadidu za rejea, Tume ilipitia na kusoma taarifa nyingi ambazo baadhi yake ni:

(i) Muhtasari wa Taarifa ya Uchambuzi wa Mikakati na Mbinu za Kupambana na Rushwa Nchini iliyotolewa na Chama Cha Mapinduzi 1989.

(ii) Taarifa ya Tume ya Shivji kuhusu Sera ya Ardhi na Mfumo wa Kumiliki Ardhi Nchini.

(iii) Taarifa za Crown Agents kuhusu taratibu za ugavi na zabuni za ujenzi serikalini.

(iv) Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali ya mwaka 1993/94.

(v) Kanuni na Taratibu za Ujenzi Nchini kama zilivyoandaliwa na Baraza la Ujenzi.

(vi) Ripoti mbalimbali za Shirika la Transparency International.

(vii) Taarifa za Shirika la Forum Against Corrupt Elements in Tanzania (FACEIT).

(viii) Taarifa ya Tume ya Rais ya Kupunguza Matumizi ya Serikali – Machi 1994.

(ix) Taarifa ya Kamati Teule ya Bunge kuhusu tuhuma dhidi ya Idara ya Wanyamapori – Novemba 1994.

(x) Taarifa ya Tume ya Mtei – 1991.

(xi) Ripoti mbalimbali za SGS na InchCape

5. Tume ilikutana na viongozi mbalimbali wa Serikali akiwamo Jaji Mkuu, majaji wa Mahakama Kuu za Kanda ya Mwanza, Tanga, Arusha na Tabora. Tume pia ilikutana na Kamati ya Uongozi ya Bunge, Kamati ya Fedha ya Bunge, Waziri wa Sheria, Mambo ya Ndani, Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Meya wa Mji wa Dodoma. Aidha ilikutana na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi, Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi na Katibu Mkuu Utumishi.

Tume pia ilikutana na Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato na wasaidizi wake, Kamishna wa Ardhi na Mkurugenzi wa Mipango Miji Wizara ya Ardhi; Mkurugenzi wa Kituo cha Uwekezaji Rasilimali; Wakurugenzi wa Idara ya Wanyamapori, Uvuvi na Misitu, Wizara ya Maliasili na Utalii; Mkurugenzi wa Biashara Wizara ya Viwanda; Maofisa Biashara na Sheria wa Jiji la Dar es Salaam, Mhandisi wa Jiji la Dar es Salaam pamoja na wahandisi kadhaa wa Wizara ya Ujenzi.

6. Tume pia ilikutana na Mkurungenzi Mkuu wa Idara ya Usalama wa 

Taifa, Inspekta Jenerali wa Polisi, Kamishna Mkuu wa Magereza na Mkurugenzi

wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa. Aidha ilikutana na viongozi wastaafu wa Idara ya Usalama wa Taifa; Polisi; Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali na Idara ya Ushuru wa Forodha ili kupata utaalamu na uzoefu wao katika mapambano dhidi ya rushwa.

7. Tume iliwaalika viongozi wa vyama vya siasa nchini ili waweze kutoa maoni yao kuhusu tatizo la rushwa nchini, lakini wito huo uliitikiwa na viongozi wa CCM, CHADEMA na UDP tu. Uongozi wa NCCR Mageuzi ulikataa wito huo kwa kueleza kwamba Tume imeundwa kwa misingi ya kibaguzi kwa kutoshirikisha vyama vya upinzani na ina sura ya CCM  na vyombo vyake.

Aidha Chama cha Wananchi (CUF) kilikataa wito huo kwa kueleza kwamba hawakushirikishwa tangu mwanzo na wanaotakiwa na Tume hiyo ni chama kilichopo madarakani, yaani CCM na wala si vyama vipya vya siasa. Kadhalika Tume ilikutana na viongozi wa baadhi ya mashirika ya umma ya TANESCO, Simu, THA na PPF, wakuu wa makampuni vya TCCIA, Dar es Salaam Chamber of Commerce, Dar es Salaam Merchant Chambers, Dar es Salaam Hunters Association, Tanzania Tour Operators.

Vile vile ilikutana na mashirika yasiyokuwa ya Kiserikali ya Forum Against Corrupt Elements in Tanzania (FACEIT) na Alcohol and Drug Information Centre (ADIC). Aidha Tume ilikutana na wananchi mbalimbali wapatao 847 ambao walijitolea kutoa maoni yao kuhusu tatizo la rushwa nchini.

8. Tume ilijigawa katika kamati ndogo ndogo ambazo zilitembelea miji mikuu ya

mikoa ya Arusha, Kilimanjaro, Morogoro, Mwanza, Mara, Kagera, Shinyanga, Kigoma, Zanzibar ambako ilikutana na wakuu wa idara mbalimbali za Serikali na mahakama, matawi ya wafanyabiashara na kupokea malalamiko na maoni ya wananchi kuhusu tatizo la rushwa mikoani mwao. Maoni haya yamesaidia sana Tume katika kutafakari ukubwa wa tatizo la rushwa nchini na hivyo kuiwezesha kutoa mapendekezo yake.

 

SHUKRANI

9.  Tume inapenda kuwashukuru wananchi wote waliotoa maoni yao ama kwa maandishi au kwa kukutana na Tume, na hivyo kuiwezesha kukamilisha taarifa hii. Aidha shukrani za dhati ziwafike viongozi wote wa Serikali waliojitolea muda wao kutoa maelezo yao kwa Tume, na wote waliosaidia kutayarisha na kufanikisha ziara za Tume mikoani.

10. Tume inapenda kutoa shukrani za pekee kwa maofisa wote wa Sekreterieti, makatibu waendesha ofisi (OMS), mwangalizi wa ofisi, dereva pamoja na wahudumu wote wa Tume ambao wameshirikiana vizuri na Tume katika kufanikisha kazi hii.

 

SURA YA PIL

HALI YA RUSHWA NCHINI

1. Katika nchi yetu kumekuwepo na onezeko kubwa la woambaji rushwa pamoja na watoaji rushwa. Taifa limeshuhudia pia ongezeko la matumizi ya madaraka kwa manufaa binafsi miongoni mwa watumishi wa umma. Wakati huo huo tabia na vitendo vya kutoheshimu sheria vimeongezeka kwa kasi kubwa.

Aidha, kumekuwepo na ongezeko la matumizi ya fedha kwa madhumuni ya kupata upendeleo katika huduma ya umma au kupinda na kuvunja sheria au taratibu kwa upande wa raia, hasa wafanyabiashara. Kwa upande wa watumishi wa umma, Tume imeridhika kwamba hali hii imetokana na kuwepo mianya, vishawishi, tamaa, uroho na uduni wa kipato katika utendaji kazi na maisha ya kila siku pamoja na mmomonyoko wa maadili, hususani katika utumishi wa umma na katika jamii kwa ujumla.

2. Hakuna utata kuwa rushwa imeshamiri katika sekta zote za uchumi, huduma na siasa nchini. Kuna ushahidi kuwa hata baadhi ya wafanyakazi wa vyombo vya dola vya Usalama wa Taifa, Polisi, Mahakama na Taasisi ya Kuzuia Rushwa vyenye jukumu la kulinda haki, wametumbukia kwenye vitendo vya rushwa. Hawa badala ya kuwa mstari wa mbele kupambana na rushwa, wamekuwa sehemu ya tatizo. Matokeo yake raia wa kawaida mpenda haki hana mahali pa kukimbilia. Amebakia kusononeka na kukosa imani na uongozi uliopo.

3. Ongezeko la rushwa katika miaka ya 1990 limechangiwa na mahusiano ya karibu kati ya wanasiasa pamoja na viongozi wengine wakuu serikalini na wafanyabiashara wenye tabia ya kutoa rushwa. Wakati wanasiasa wanafanya maamuzi yaliyozua hisia za rushwa, wafanyabiashara wametumia uhusiano wa karibu uliopo kuendeleza masilahi yao kibiashara. Wakati mwingine maamuzi ya kisiasa yamechukuliwa bila kuzingatia masilahi ya Taifa.

4. Watoaji rushwa wamegawanyika katika makundi mawili. Kwanza, ni kundi la matajiri wanaohonga kushawishi watumishi wa umma wapinde au wavunje sheria, taratibu au kanuni ili kuendeleza masilahi yao. Kundi la pili ni la wale wanaolazimika kutoa hongo kutokana na shinikizo la watoa huduma. Hawa wanajikuta wakilazimika kutoa hongo ili wapate huduma. Hili ni kundi la watu safi, lakini mazingira yanawafanya washawishike kushiriki katika vitendo vya rushwa.

5. Kundi la kwanza la watoaji rushwa ni kundi hatari sana, na vitendo vyao vina athari kubwa katika mfumo wa maamuzi na utendaji kazi katika sekta ya umma. Kutokana na shinikizo lao, mtiririko wa utendaji kazi, haki na malengo ya kitaifa ya kisiasa na kiuchumi hupotoshwa. Kushamiri kwa kundi hili kunaashiria kujengeka kwa tabaka katika jamii na kuzusha mmomonyoko wa mshikamano.

6. Kwa upande wa wapokeaji ambao ni watumishi wa umma wenye mamlaka ya kufanya maamuzi au walio katika nafasi za kuweza kushawishi maamuzi au kutoa huduma, nao pia wamegawanyika katika makundi mawili. Walio katika kundi la kwanza ni wale ambao kupokea kwao rushwa ni matokeo dhahiri ya hali duni kifedha na kimaisha kwa ujumla na wanachopokea husaidia tu kuziba pengo hilo. Aina hii ya rushwa ndiyo inayowakera sana wananchi wa kawaida mijini na vijijini na imeenea katika   sekta zote za umma kama ifuatavyo:

 

ELIMU:

(i) Wazazi kudaiwa rushwa na baadhi ya walimu ili waweze kuwaandikisha watoto wao shuleni na wakati mwingine kwa visingizio kuwa ni michango.

(ii) Walimu hutoa rushwa kwa maofisa elimu wa wilaya, mikoa na wizara ili waweze kupandishwa vyeo.

(iii) Rushwa hutolewa kwa walimu ili kuwawezesha wanafunzi kushinda mitihani ama kwa kuwaongezea maksi, kubadili namba za mitihani au kufanyiwa mitihani na walimu au vijana wa shule za sekondari.

(iv) Rushwa hudaiwa au kutolewa kwa walimu ili kuwawezesha wanafunzi wasiokuwa na uwezo kupata nafasi za masomo ya sekondari na vyuo.

(v) Rushwa hudaiwa na kutolewa kwa maofisa wa Wizara ya Elimu na walimu wakuu ili kuwapatia wanafunzi uhamisho, nafasi ya kurudia darasa.

(vi) Rushwa hutolewa kwa ajili ya upatikanaji wa nafasi ya malazi ya hosteli na mabweni katika shule za sekondari, vyuo na vyuo vikuu.

(vii) Walimu ama kwa ridhaa yao au kwa kudaiwa, hutoa rushwa ili wahamishwe au wasihamishwe sehemu zao za kazi.

(viii) Rushwa hutolewa kwa wale wanaokwenda kusahihisha mitihani ili waongeze maksi za kufaulu mitihani ya watoto waliotahiniwa na hivyo kushinda isivyo halali.

(ix) Wanawake wanaosoma vyuoni na vyuo vikuu hudaiwa na kutoa rushwa ya mapenzi ili waweze kufaulu mitihani yao.

 

AFYA

(i) Rushwa hudaiwa katika zahanati, vituo vya afya na hospitali ambapo wagonjwa au ndugu zao wanalazimishwa kutoa fedha kwa wahudumu, manesi na madaktari ili waweze kupatiwa huduma.

(ii) Rushwa hutolewa ili kukiuka utaratibu uliowekwa makusudi kwa ajili ya kuweza kuwaona madaktari, kupata vitanda katika wodi na wodi za wazazi, kupata madawa, matibabu, huduma za maabara na x-ray, kuwepo katika orodha ya kufanyiwa upasuaji na kupata idhini na fedha za matibabu nje ya nchi.

(iii) Madaktari hutoa rushwa kwa watendaji wakuu ili wahamishwe au wasihamishwe mikoa au hospitali wanazotaka au wasizozitaka.

(iv) Mabwana na mabibi afya wadhibiti wa chanjo ya watu wanaoingia nchini, huomba na kupokea rushwa ili waruhusu au waruhusiwe kukwepa taratibu za afya zinazotawala wanaoingia nchini.

(v) Wahudumu wa vyumba vya maiti hudai na kupokea rushwa kwa kuhifadhi, kuandaa na kutoa maiti.

 

MAMBO YA NDANI:

Polisi:

(i) Askari wa Usalama Barabarani hulipwa kiasi maalumu kila siku na madereva wa daladala ili wasiwakamate wanapovunja sheria.

(ii) Rushwa hutolewa na madereva kwa polisi wanapopatikana na makosa barabarani.

(iii) Polisi hudai rushwa toka kwa watu wanaotuhumiwa kwa uhalifu ili wasiwakamate au kuwafungulia mashtaka.

(iv) Polisi huwakamata watu na kuwasingizia makosa ya uongo kama namna ya kushawishi rushwa. Kwa mfano sehemu za mijini watu wanaotoka kutembea usiku husingiziwa makosa ya kuwa na bangi au madawa ya kulevya. Huko vijijini, watu wamekuwa wanafunguliwa makosa ya uongo na mwishowe kudaiwa kutoa kitu chochote kama ng’ombe ili kesi zao zifutwe.

(v) Polisi hupokea rushwa kutoka kwa watu wanaoingia katika viwanja vya michezo, hususan Uwanja wa Taifa Dar es Salaam kwa ajili ya kuona mapambano ya mpira wa miguu badala ya watu hao kulipa viingilio vilivyopangwa na kupewa stakabadhi halali.

(vi) Polisi hupokea rushwa kutoka kwa wahalifu ili wasiwafichue.

(vii) Polisi huwafungulia watu mashtaka mazito ya makosa yenye adhabu kubwa ili watuhumiwa watoe rushwa na hivyo uzito wa mashtaka yao kupunguzwa.

(viii) ‘Public Prosecutors’ wanapokea rushwa ili kuleta mashahidi wa kubabaisha mahakamani.

(ix) Polisi katika vizuizi hupokea rushwa na kuruhusu mazao kutoroshwa kwenda nchi jirani.

(x) Wapelelezi wa Polisi huchelewesha shughuli za upelelezi ili kuwalazimisha wenye kesi kutoa rushwa.

 

UHAMIAJI:

(i) Maofisa Uhamiaji hudai na kupokea rushwa kutoka kwa raia katika kushughulikia pasi za kusafiria.

(ii) Rushwa hudaiwa na hutolewa kwa maofisa Uhamiaji ili kuwapa uraia, pasi za kusafiria, viza na vibali vya kuishi nchini watu wasiostahili.

 

MAGEREZA:

(i) Askari Magereza hudai rushwa ili kutoa huduma kwa upendeleo kwa wafungwa na mahabusu. Wenye uwezo wa fedha hupewa chakula kizuri, kazi laini na matandiko mazuri ya kulalia.

 

FEDHA:

(i) Wahasibu hudai rushwa ili kuidhinisha na kupitisha malipo ya wafanyakazi wenzao.

(ii) Maofisa wa Hazina hudai rushwa ili watoe fedha zilizoidhinishwa na Bunge kwa maofisa wahasibu wa wizara na mikoa.

(iii) Wateja hudaiwa rushwa ili kupata na kurejesha mikopo kutoka mabenki.

(iv) Rushwa hutolewa wakati wa makadirio na malipo ya kodi na ushuru na pengine kusamehewa kodi.

(v) Rushwa hutolewa kwa watendaji wa wizara, idara na mashirika ya umma ili kupata idhini ya malipo baada ya kuwasilisha mali au huduma.

(vi) Wakaguzi wa hesabu hudai rushwa ili kuficha madhambi mbalimbali wanayoyagundua wakati wa ukaguzi.

(vii) Wastaafu na watu walioachishwa kazi hudaiwa rushwa ili waweze kupata malipo yao ya uzeeni.

(viii) Rushwa hutolewa na wateja wasiostahili kulipwa Bima ili hoja zao za ma 

(Ripoti tuliyoipata sehemu hii imekatika)

na kupokea rushwa na kuwaachia wavuvi wanaokamatwa wakivua ama waliovua samaki kwa kutumia baruti au madawa kama DDT au nyavu zisizoruhusiwa.

(iv) Rushwa hutolewa kwa maofisa wanyamapori wakati wa kugawa vitalu vya uwindaji.

(v) Maofisa wanyamapori hupokea rushwa ili kutoa Presidential Hunting Licences kwa watu wasiostahili.

 

Je, unajua ni makundi yapi mengine aliyataja kuwa wala rushwa nchini na mbinu wanazotumia kuchukua rushwa? Wiki ijayo usikose sehemu ya pili ya mfulululizo wa machapisho ya Ripoti ya Rushwa ya Jaji Warioba ya Mwaka 1996 inayochapishwa na Gazeti la JAMHURI pekee, linaloanzia wanapoishia wengine.

By Jamhuri