Na Mwandishi Wetu
MRADI wa Uendelezaji Miundombinu ya Miji Tanzania (TACTIC) unaelezwa kuimarisha huduma za usafiri na usafirishaji katika Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga mkoani Rukwa baada ya ujenzi wa miundombinu ya barabara.
Hayo yamebainishwa na Kaimu Mkurugenzi Manispaa ya Sumbawanga, Nassir Kilusha ambapo amesema kuwa kiasi cha shilingi Bilioni 20.361 zimepokelewa kupitia mradi wa TACTIC kwa ajili ya ujenzi wa jengo la ofisi kwa wasimamizi wa mradi, ujenzi wa barabara zenye urefu wa Kilomita 13.3 kwa kiwango cha lami, ujenzi wa mitaro pamoja na uwekaji wa taa za barabarani ambapo utekelezaji wake umefikia asilimia zaidi ya 80.

“Kabla ya mradi barabara zilikuwa na vumbi, mashimo, matope na maji kujaa katika makazi ya watu na kusababisha kero kwa wananchi lakini sasa maji hayatuami kutokana na mitaro, biashara zinafanyika hadi usiku kwasababu ya taa, uwekezaji umeongezeka, usalama umeongezeka, thamani ya viwanja na nyumba imepanda pia shughuli za usafiri na usafirishaji zimeongezeka”, amesema.
Kilusha ameongeza kuwa sasa wanaendelea na ujenzi wa Soko kuu la mazao ya nafaka eneo la Kanondo ambalo litaongeza thamani ya mazao likijumuisha maegesho ya magari, eneo la mawakala, maghala ya kuhifadhia mazao na eneo la kuuzia chakula (baba lishe na mama lishe) kwa gharama ya shilingi Bilioni 7.4 ujenzi unaotarajiwa kukamilika Desemba 2025.
Kuhusu mapato ya Halmashauri, Kilusha ameeleza kuwa mwaka wa fedha uliopita walikuwa wanakusanya shilingi Bil. 3.4 lakini mwaka huu wa fedha wanatarajia kukusanya shilingi Bil. 3.9 kutakuwa na ongezeko la shilingi mil. 500 ambapo amewataka wananchi kuilinda miundombinu hiyo ili iweze kudumu kwa muda mrefu.

Kwa upande wake, Mratibu wa TACTIC kutoka TARURA wilaya ya Sumbawanga, Mhandisi Emmanuel Kudema amesema kabla ya mradi wa TACTIC walikuwa na barabara za lami Km 32.89 lakini baada ya mradi zimejengwa Km 13.03 na kufanya zifikie Km 45.92 za lami ambazo zimepunguza matengenezo ya mara kwa mara na kuboresha mtandao wa barabara.
Naye, Nasma Kazumari mkazi wa kata ya Katandala ameishukuru Serikali kwa ujenzi wa barabara sasa wanafanya biashara hadi usiku sababu ya taa, wateja wameongezeka, mji umekuwa msafi tofauti na awali barabara zilikuwa na vumbi, matope na mazingira machafu ambapo kiafya haikuwa nzuri.
Baraka Edwin, Mkazi wa kata ya Mafulala ambaye ni dereva bajaji amesema mwanzoni walikuwa wanatumia muda mrefu kuzunguka lakini sasahivi barabara nzuri wanapata abiria wengi na hawatumii muda mrefu njiani, pia amewaomba wananchi wenzake kuitunza miundombinu hiyo kwa kutotupa taka kwenye mitaro ili isizibe na maji kujaa barabarani.

Kwa upande wake, Getricia Bomani ambaye amepata ajira ya kutoa huduma ya kwanza katika ujenzi wa soko la Kanondo ameishukuru Serikali kwa mradi huo kwani ajira aliyoipata inamsaidia kujikwamua kiuchumi na kusaidia familia pia amesema soko hilo likikamilika litaongeza thamani ya mazao na kuuza mazao nchi za jirani kama Congo na Zambia.



