Na Mwamvua Mwinyi, JamhuriMedia, Pwani
MWENYEKITI wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Mkoa wa Pwani ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa huo, Abubakar Kunenge, ameagiza askari polisi kujitathmini kwa kuzingatia utii, weledi na haki katika utekelezaji wa majukumu yao.
Kunenge alitoa maelekezo hayo April 30,2026 alipokuwa akizungumza katika Siku ya familia ya Polisi iliyofanyika katika viwanja vya Fire, Kibaha,ambapo kulitolewa na tuzo kwa baadhi ya maafisa ukaguzi na askari waliofanya vizuri .
Alisisitiza umuhimu wa kuimarisha usalama kwa kushirikiana na vyombo vingine pamoja na wananchi, akieleza kuwa mafanikio ya kiuchumi na uwekezaji hayawezi kupatikana endapo kutakuwepo vitendo vya uhalifu kama wizi na utapeli.
“Ni lazima tushirikiane na jamii katika kulinda usalama, Huwezi kuwa na uwekezaji kama kuna wizi au utapeli, mafanikio haya tunayojivunia yanatokana na kazi kubwa inayofanywa na Jeshi la Polisi mkoani hapa,” alisisitiza Kunenge.
Aidha, alieleza kipindi cha nyuma kulikuwa na viwanda 1,357 kwasasa vimefikia 1,722 kati ya hivyo 269 vimejengwa kipindi cha awamu ya sita ambapo amepongeza Jeshi hilo kwa kazi nzuri ya kulinda raia na mali zao.
Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Salim Morcase, alisema maafisa na askari waliotunukiwa zawadi wameonesha utendaji mzuri, na kwamba tuzo hizo zinalenga kuongeza ari kwa wengine kufanya kazi kwa bidii .
Aliongeza kuwa jeshi hilo linathamini mchango wa wadau mbalimbali wanaoshirikiana nalo katika shughuli za ulinzi na usalama, huku akimshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuboresha mazingira ya kazi kupitia utoaji wa vitendea kazi ikiwemo magari, ujenzi wa vituo vya polisi katika maeneo kama Bagamoyo na Kisarawe na ukarabati wa majengo chakavu.









