Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dar es Salaam

Baraza la Wasafirishaji Shehena Tanzania (TSC), limefurahia uamuzi wa serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) kwa kukubali kupunguza Tozo ya Uendelezaji wa Miundombinu ya Bandari (Port Infrastructure Development – PID) kwa asilimia 50, kutoka asilimia tisa (9%) hadi 4.5% ya thamani ya forodha.

Akizungumza na wanahabari, Mwenyekiti wa TSC, Bw. Clement William Kamendu, amebainisha kuwa tozo hiyo mpya ambayo sasa itaanza kutumika rasmi tarehe 1 Julai, 2026 kufuatia kuahirishwa kwa miezi michache itasaidia wadau wa bandari kujipanga.

Bw. Kamendu ametoa hesabu ya haraka kuonesha jinsi usikivu wa TPA ulivyookoa mamilioni ya fedha kwa wafanyabiashara akieleza kuwa kwa shehena yenye thamani ya Shilingi bilioni moja, tozo ya awali ya 9% ingewalazimu wafanyabiashara kulipa Shilingi milioni 90. Kutokana na punguzo hilo la nusu hadi 4.5%, sasa watakuwa wakilipa Shilingi milioni 45 tu.

Bw. Kamendu ametoa wito kwa wafanyabiashara na wasafirishaji wote kutoa ushirikiano wa dhati kwa TPA na serikali kwa kulipa tozo hizo kwa wakati ili kuboresha huduma. Amesisitiza kuwa lengo kuu ni kupunguza gharama za usafirishaji na ugavi ambazo kwa Afrika ziko juu.