Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dodoma

Wadau wa Sekta ya Madini wamehimizwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zinazosimamia shughuli za madini ili kuhakikisha rasilimali hizo zinaendelea kuchangia maendeleo ya taifa na kunufaisha wananchi.

Mwanasheria wa Tume ya Madini, Janeth Kanyasu, amesema hayo kwenye Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali Park mkoani Dodoma, ambapo Tume inaendelea kutoa elimu kwa wananchi na wadau mbalimbali kuhusu masuala ya Sekta ya Madini.

Amesema elimu hiyo inahusu Sheria ya Madini Sura ya 123 na kanuni zake, ikijumuisha utoaji wa leseni mbalimbali, biashara ya madini, uwekezaji, shughuli za uchimbaji na usimamizi wa mazingira ili kuhakikisha rasilimali za madini zinatumika kwa tija na kwa kuzingatia matakwa ya sheria.

“Kuzingatia sheria na taratibu zilizowekwa ni msingi wa kuhakikisha Sekta ya Madini inaendeshwa kwa uwazi, uadilifu na kuendelea kutoa manufaa kwa taifa na wananchi,” amesema Kanyasu.

Amesema pia wananchi wanaelimishwa kuhusu ushiriki wa Serikali katika shughuli za madini, ushirikishwaji wa Watanzania katika sekta hiyo kupitia sera ya Ushiriki wa Watanzania katika Sekta ya Madini pamoja na utekelezaji wa miradi ya uwajibikaji kwa jamii (CSR) inayotekelezwa na kampuni za madini.

Kwa mujibu wa Kanyasu, Tume ya Madini inaendelea kutoa ufafanuzi kuhusu ulipaji wa mirabaha na tozo mbalimbali zinazotakiwa kisheria, ikiwemo Service Levy, HIV Levy, mrabaha wa madini ya ujenzi wa asilimia tatu, madini ya metali asilimia sita na ada ya ukaguzi ya asilimia moja.

Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma mwaka huu yanaongozwa na kaulimbiu isemayo, “Kuchochea Uwajibikaji Jumuishi kwa Huduma Endelevu,” na yanatarajiwa kuhitimishwa Juni 23, 2026