ARUSHA

Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP Centre) kinatarajiwa kufanya mhadhara wa umma utakaolenga kujadili mchango wa ubia kati ya sekta umma na sekta binafsi katika kuchochea maendeleo ya watu na uchumi wa taifa.

Mhadhara huo utaongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa PPP Centre, Mhe. David Kafulila ukiwa umebeba mada ya “Ubia Kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP) kama Nyenzo ya Kuchochea Maendeleo ya Watu: Fursa katika Mpango wa Nne wa Maendeleo (FYDP IV) na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.”

Mhadhara huo unatarajiwa kufanyika tarehe 14 Agosti 2026 kuanzia saa 3:00 asubuhi katika ukumbi wa Taasisi ya Maendeleo ya Jamii Tengeru(TICD) jijini Arusha, na unatarajiwa kuwahusisha wanafunzi, wahadhiri na wadau kutoka sekta ya umma, sekta binafsi pamoja na washirika wa maendeleo.

Aidha, mhadhara huo unalenga kuongeza uelewa kuhusu nafasi ya ubia wa PPP katika kuharakisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo, kuvutia uwekezaji na kuchochea ukuaji wa uchumi unaowanufaisha wananchi, sambamba na malengo ya FYDP IV na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.