Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dar es Salaam
Mbuzi wa Benki ya NMB, ‘NMB the GOAT’, ameibuka mshindi katika mbio za ‘NMB unGOATable Race’ zilizofanyika Septemba 19, 2026, akimshinda mbuzi wa Bowman katika mashindano Goat Races yanayolenga kuchangisha Sh200 milioni kwa ajili ya kusaidia elimu ya juu kwa vijana 150. NMB imeshiriki kwa mara ya kwanza kama mmoja wa wadhamini wakuu wa mashindano hayo.
Akizungumza baada ya ushindi huo, Mkuu wa Idara ya Huduma za Kibenki kwa Wateja Maalumu wa NMB, Getrude Mallya, alisema ushindi wa mbuzi huyo umefanya ushiriki wa kwanza wa benki katika mashindano hayo kuwa wa kipekee. Alisema NMB inajivunia kuunga mkono tukio linalounganisha burudani na uchangishaji wa fedha kwa ajili ya kuwasaidia vijana wenye changamoto za kifedha kuendelea na masomo.
“Zaidi ya furaha ya ushindi, ushiriki wetu katika mashindano haya unaakisi dhamira ya Benki ya NMB ya kuunga mkono jitihada zinazofungua fursa kwa vijana wa Kitanzania. Mashindano haya yanatuunganisha kwa lengo muhimu la kuchangisha fedha kusaidia elimu,” alisema Mallya.
Kwa mujibu wa Rais wa Rotary Club ya Dar es Salaam Oysterbay, Paul Muhato, wanafunzi 350 wamewezeshwa kuendelea na masomo tangu klabu hiyo ilipoanza kusimamia rasmi mashindano hayo mwaka 2018. Mashindano ya mwaka huu yanalenga kuongeza idadi hiyo kwa kuwawezesha wanafunzi wengine 150 kupata elimu ya juu mwaka ujao.









