Na Mwandishi Wetu,JamhuriMedia,Tabora

Kulwa Paulo Chamkoko, mkazi wa mtaa wa Ghana Kata ya Kiloleni ,Manispaa ya Tabora amehukumiwa kifungo cha maisha jela baada ya kutiwa hatiani kwa kosa la kumbaka mtoto wa miaka tisa.

Adhabu hiyo imetolewa na Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Wilaya ya Tabora, John Christopher Mdoe, baada ya kuridhika na ushahidi usioacha shaka uliotolewa na upande wa mashitaka.

Hakimu Mdoe amesema ushahidi uliotolewa mahakamani na mashahidi nane wa upande wa mashitaka akiwemo mhanga wa tukio hilo na ule wa daktari umethitisha pasipo shaka kwamba mshitakiwa ndiye alitenda kosa hilo Juni 15,2021.

Awali upande wa Jamuhuri ukiongozwa na wakili wa Jaines Kihwelo ulidai mahakamani hapo kuwa mshitakiwa alitenda kosa hiloo Juni 15,2021, majira ya saa 7, mchana na saa 4, usiku mtaa wa Ghana, Kata ya Kiloleni mjini Tabora.

Ilidaiwa kuwa siku hiyo mlalamikaji ambaye jina limehifadhiwa mwanafunzi mwenye umri wa miaka tisa baada ya kutoka shule majira ya saa 7 mchana, alitumwa na bibi yake kwa jirani yake lakini alirejea maira ya saa 4 usiku.

Upande mashitaka uliongeza kuwa mshitakiwa ndiye aliyemsindikiza nyumbani kwao mtoto huyo ambapo alimdanganya bibi yake kwamba amemkuta njiani ndipo akaamua kumsindikiza kwani ilikuwa ni usiku.

Inadaiwa kuwa shangazi wa mtoto huyo ambaye ni miongoni mwa mashahidi mara baada ya kumhoji na kumfanyia upekuzi alikuta sehemu za siri zikiwa zimevimba pamoja na damu iliyoganda.

Chamkoko katika utetezi wake alidai kuwa kulikuwa na kutoelewana baina yake na bibi wa mtoto huyo kwani aliwahi kumtamkia maneno kwamba atampoteza kama ilivyotokea.

Aliiomba mahakama itumie vipimo vya DNA kuweza kuthibitisa kosa lake hoja ambayo ilitupiliwa mbali kwa kukosa mashiko ya kisheria.

Akitoa hukumu ya kesi hiyo Hakimu Mdoe alisema kwa kuzingatia matakwa ya sheria inaelekeza kwamba endapo mhanga ni mtoto chini ya miaka kumi adhabu kwa mkosaji ni moja tu ambayo ni kifungo cha maisha jela.

By Jamhuri