LONDON - APRIL 21: Arsenal manager, Arsene Wenger looks on during the Barclays Premiership match between Tottenham Hotspur and Arsenal at White Hart Lane, on April 21, 2007 in London, England.  (Photo by David Cannon/Getty Images) *** Local Caption *** Arsene Wenger
LONDON – APRIL 21: Arsenal manager, Arsene Wenger looks on during the Barclays Premiership match between Tottenham Hotspur and Arsenal at White Hart Lane, on April 21, 2007 in London, England. (Photo by David Cannon/Getty Images) *** Local Caption *** Arsene Wenger
Mashabiki wa Washika Bunduki wa England – Arsenal ‘the Gunners’, wana imani na timu yao, ndiyo maana katika mechi tatu za Ligi Kuu England, licha ya kutokuwa na matokeo ya kufurahisha, wamekuwa wakishangilia tu kwa kuimba “Tunaipenda Arsenal, Tunaipenda…”

Kwa mashairi hayo kama ingekuwa Tanzania, bila shaka yangefanana na sehemu ya beti za moja ya nyimbo za bendi ya African Stars ‘Twanga Pepeta’, inayoimbwa ‘Ninavyokupenda Arsenal, nitakunywa sumu juu yako.”

Lakini pamoja na shangwe hizo, Arsenal inaweza kuweka rekodi ya kutotwaa taji la Ligi Kuu ya England kwa mwaka wa 12 mfululizo. Mara ya mwisho, imetwaa taji hilo 2004 ingawa hapa katikati angalau imetwaatwaa taji la Kombe la FA maarufu kama CapitalOne, lakini Ligi Kuu imekuwa fupa gumu.

Matumaini ya The Gunners kutwaa taji la ligi hiyo msimu huu, yameanza kupotea licha ya kuanza vema msimu huu.

Nafasi yake ilikuwa kubwa kwa kuwa washindani wake kama Chelsea, Manchester City, Liverpool na Manchester United hawakuwa mahiri ikilinganishwa na vijana hao wa Meneja Wenger.

Arsenal kama haikutwaa ubingwa msimu huu itabidi ijilaumu tu kama Liverpool msimu uliopita. Liverpool ilifanya vema hadi dakika za mwisho kama Arsenal sasa, lakini ikashindwa kutwaa taji.

Kupoteza mechi zake mbili mfululizo zilizopita na kutoka sare ya mabao 2-2 na Tottenham Jumamosi iliyopita, bila shaka ni dalili mbaya kwa Washika Bunduki hao wa Kaskazini London.

Kabla ya sare hiyo, ililazwa mabao 2-1 na Swansea uwanjani Emirates Jumatano na kabla ilifungwa na Manchester United kwenye dimba Old Trafford.

Kutokana na kufungwa huko, Kocha wa Arsenal, Arsene Wenger, ana wasiwasi kuhusu matokeo ya timu yake. Anasema wachezaji wake wanafaa kuimarika baada ya kufungwa na sare ya Jumamosi iliyopita.

Lakini mshambuliaji wa kati wa Arsenal, Alexis Sanchez, amesema kuwa Arsenal haina nafasi tena ya kutwaa taji la Ligi Kuu baada ya kufungwa mfululizo na Manchester United na Swansea na kutoka sare na Tottenham.

“Mara nyingi tunakosa ari baada ya kuongoza 1-0 uwanjani,” anasema Sanchez na kuongeza: “Tunakosa ile ari na kujikuta tunafungwa, na hii ni mbaya kwani tunaweza kupoteza nafasi ya ubingwa. 

Anasema: “Iwapo tutaingia katika uwanja na ari ya kuwa mabingwa, kushinda ligi ama hata Ligi ya Mabingwa Ulaya, tunaweza kufikia hilo. Ninakumbuka mechi dhidi ya Manchester United mwaka uliopita. Wachezaji walikuwa na ari ya kushinda taji tulipoingia uwanjani. Tuliwashinda katika dakika 20 na kupata 3-0. Tulikuwa na ari na kujiamini siku hiyo.”

Arsenal imeshinda mara tatu tu katika mechi 11 katika mashindano yote na wako katika nafasi ya tatu katika ligi.

Timu hiyo sasa imepungua nguvu baada ya kipa wake mahiri, Petr Cech, kuumia dakika za majeruhi katika mchezo dhidi ya Swansea City na Wenger anasema ni bahati mbaya.

“Zaidi Cech alikuwa ana tatizo na mtoki kabla ya mechi na katika mchezo alihaha sana,” anasema Wenger na kuthibitisha kwamba watamkosa kipa huyo kwa wiki tatu hadi wiki nne kutokana na maumivu hayo.

Kipa huyo mwenye umri wa miaka 33 atakosa mechi tatu za Ligi Kuu, pamoja na mechi muhimu ya Ligi ya Mabingwa Ulaya itayochezwa Camp Nou dhidi ya Barcelona. 

Aidha, atakosa mechi ya marudiano Kombe la FA dhidi ya Hull. Pia itamkosa beki Laurent Koscielny kutokana na maumivu ya mguu. Koscielny (30), pia hakuchezea mechi dhidi ya Swansea.

The Gunners au Washika Bunduki wamo kwenye nafasi ya tatu katika msimamo wa Ligi Kuu, alama sita nyuma ya vinara Leicester, na alama tatu nyuma ya Tottenham wanaoshika nafasi ya pili.

By Jamhuri