Baada ya kuchaguliwa kuwa Kaimu Katibu Mkuu wa Yanga akichukua nafasi ya Charles Mkwasa, Omary Kaaya, ameibuka na kueleza jambo la kwanza ambalo Wanayanga kwa ujumla wanapaswa kulitilia nguvu.

Kaaya amesema ili Yanga iweze kusonga mbele cha kwanza inabidi waunganike wawe wamoja ili kuijenga klabu iweze kusimama vizuri ili iweze kuzidi kutengeneza heshima kubwa nchini na nje ya Tanzania.

Kaaya ameamua kufunguka hayo kutokana na baadhi ya viongozi wa klabu hiyo kutokuwa na maelewano, jambo ambalo limesababisha baadhi ya waliokuwa katika Kamati ya Utendaji ikiwemo Khalfan Hamis kuachia ngazi.

Kaaya ameeleza Yanga kwa sasa inapitia changamoto nyingi hivyo ni vema wanachama na mashabiki wake wakasahau hayo na kuweka silaha chini ili wawekeze nguvu zao ndani ya klabu kwa sasa.

Wakati Kaaya akifunguka hayo, Yanga inashuka kibaruani Jumapili ya wiki hii kucheza mchezo wa Kombe la Shirikisho wa mkondo wa pili dhidi ya Gor Mahia FC kwenye Uwanja wa Taifa.

Yanga itaingia kucheza na Gor Mahia baada ya kupoteza mechi ya kwanza kwa kufungwa mabao 4-0 ugenini, Nairobi, Kenya wiki jana.

By Jamhuri