BABU SEYA: TUNAANDAA MAMBO MAKUBWA MASHABIKI TULIENI

NGULI wa muziki wa dansi, Nguza Vicking ‘Babu Seya’ na mwanaye Jonhson Nguza ‘Papii Kocha’ kwa mara ya kwanza tangu waachiwe huru Desemba 9 kwa msamaha wa Rais John Maguuli, leo Januari 5 wamekutana na Naibu Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Juliana Shonza pamoja na wanahabari ambapo wamepata fursa ya kueleza namna walivyojipanga kurudi kwenye tasnia ya muziki.

Akizungumza na wanahabari katika Studio za Wanene Entertainment zilizopo Mwenge, Coca-cola, Naibu Waziri Shonza amesema wao kama wizara kazi yao kubwa ni kuwasaidia wasanii na kuhakikisha wanafanikiwa kufikia malengo yao, hivyo wameamua kuwakutanisha na wadau wa muziki wakiwemo Wanene ili kufanmikisha zoezi la nguli hao kurudi kwenye game.

“Sisi kama wizara kuna namna ambayo tunaitumia kuwasapoti wasanii, hatuwezi kutoa fedha, hivyo tumeamua kuwakutanisha Babu Seya, Papii Kocha na Studio ya Wanene ili waweze kuweka mipango sawa kwa ajiri ya kuendeleza muziki,” alisema Shonza.

Kwa upande wake Babu Seya alisema mashabiki wao watulie kwani mipango ndiyo inapikwa hivyo mambo yakikamilika kila kitu watakiweka hadharani.

“Baada ya shooting na recording tutaangalia namna ya kufanya lakini hatutakuwa na utaratibu wetu wa zamani wa kupiga shoo kila siku,” alisema Babu Seya huku papii Kocha akiachia kionjo cha moja ya wimbo wao wa zamani.

Aidha, Mmiliki wa Studio za Wanene, Dash alisema wao wamejipanga kutoa sapoti ya ainza zote kwa babu Seya na papii ili kuhakikisha wanarekodi kazi nzuri na kuzifikisha kwa jamii na mashabiki wao.