Barack Hussein Obama ni nani?

 

Barack Hussein Obama alizaliwa Agosti 4, 1961. Ni Rais wa 44 na Rais wa sasa wa Marekani. Ni Raia wa Marekani na Rais wa kwanza mwenye asili ya Afrika kushika wadhifa huo. Pia ni mtu wa kwanza aliyezaliwa Hawaii kushika nafasi hiyo.

Alianza kampeni za urais mwaka 2007 na mwaka 2008. Kwa mara ya kwanza alichaguliwa kuwa Rais wa Marekani mwaka 2009 na baadaye tena Januari 2013, baada ya kumshinda mpinzani wake kutoka Chama cha Republican, Mitt Romney.

 

Mei 2012, Rais Obama aliweka rekodi ya kuwa Rais wa kwanza wa Marekani kukubali ndoa za jinsia moja.

 

Baba yake Obama

Baba mzazi wa Barack Obama ni wa kabila la Waluo kutoka Nyang’oma, Kogelo nchini Kenya. Wazazi wa Obama walikutana mwaka 1960 wakati wakiwa masomoni katika Chuo Kikuu cha Hawaii, wakati baba yake alipopata nafasi ya kusoma nchini Marekani.

 

Walioana Februari 2, 1961 katika Kijiji cha Wailuku na kutengana muda mfupi baada ya Barack Obama kuzaliwa. Mzee Obama alihitimu shahada yake ya Uchumi mjini Hawaii Juni 1962 na baadaye alirudi Kenya  mwaka 1964.

 

Baba yake alimtembelea Barack mjini Hawaii mara moja mwaka 1971. Alifariki kwa ajali mwaka 1982. Mwaka 1963, mama yake Obama, Dunham, alikutana na kuoana na raia wa Indonesia, Lolo Soetoro, mjini Molokai Machi 15, 1965, hivyo Obama kuhamia Jakarta.

 

Mwaka 1971, Obama alirudi na kuishi bibi na babu yake, Madelyn na Stanley Dunham, na kujiunga na Chuo cha Maandaliazi cha Punahou hadi alipohitimu masomo yake 1979.

 

Obama aliishi na mama na dada yake mjini Hawaii mwaka 1972 hadi 1975 wakati  mama yake alipohitimu anthropologia (masomo yahusuyo binadamu) katika Chuo Kikuu cha Hawaii.

 

Mama yake Obama alipata shahada ya PhD mwaka 1992 kabla ya kufa mwaka 1995 katika mji wa Hawaii, baada ya kuugua ugonjwa wa kansa kizazi.

 

Vituko vya Obama akiwa mtoto

Obama hakuwahi kuficha historia ya maisha yake aliyoyaandika katika kitabu cha makuzi yake ya utotoni kuwa aliwahi kutumia pombe, bangi na dawa za kulevya. Pia alikuwa mwanachama “choom gang”, kikundi kilichojihusisha na matumizi ya uvutaji bangi.

 

Katika kitabu hicho anasema, “Nilidunduliza nikaweza kununua suti na viatu vilivyonibana, ofisini walishangaa! Wakati tukiendelea na masomo yetu ya sheria mimi na Michelle tulifanya kazi katika Kampuni ya Uwakili ya Sidley na Austin jijini Chicago.

“Binafsi nilikuwa na wasiwasi kuhusu ujana wangu na hasa changamoto kuwa maisha ya sasa ni fedha. Hofu yangu ilikuwa ni lini nitaanza kukamata fedha nyingi ili zisaidie kufikia mahala ninapotaka.

“Lakini kutokana na kupanda kwa gharama na mikopo niliyochukua serikalini kwa ajili ya masomo, niliamua kuendelea kuwatumikia mabwana wawili – chuo na kampuni ya sheria.

 

“Nilijitahidi kadiri nilivyoweza kudunduliza sehemu ya kipato changu. Hatimaye nilifanikiwa kuwa na chumba. Nilinunua suti zangu tatu na pia jozi moja ya viatu.

“Hata hivyo, wakati nanunua viatu sikuwa makini kwani vilionekana vidogo; vilivyonibana na kunifanya nionekane mshamba. Siku niliyoripoti ofisini, kila mmoja aliniangalia. Ingawa sikujua ni kwa nini, nilihisi walifanya hivyo kutokana na viatu vyangu!”

 

Kutembelea ndugu

Februari 1981 na katikati ya mwaka 1981, Obama alisafiri kwenda kumtembelea mama yake na dada wa kambo, Maya, na pia aliwatembelea rafiki zake aliosoma nao katika nchi ya Pakistan na India kwa wiki tatu. Alikwenda Kenya Agosti 2006 kwa ajili kusalimia ndugu na jamaa katika kijiji alichozaliwa baba yake mjini Kisumu.

 

Awali Obama alifanya kazi kama Seneta mdogo kutoka Jimbo la Illinois, tangu Januari 2005 hadi alipojiuzulu baada ya kushinda uchaguzi wa Rais wa Marekani Novemba 2008.

 

Obama alifuzu masomo katika Chuo Kikuu cha Columbia, kisha kufuzu katika Kitivo cha Masomo ya Sheria Chuo Kikuu cha Harvard, ambako alikuwa Rais wa Jarida la Harvard Law Review. Baadaye alifanya kazi kama mwanaharakati wa mambo ya kijamii kabla ya kuhitimu masomo ya sheria.

 

Alifanya kazi kama Wakili wa Haki za Umma mjini Chicago, kisha akafundisha Sheria ya Katiba katika Chuo Kikuu cha Chicago kuanzia mwaka 1992 hadi 2004.

 

Obama alifanya mihula mitatu katika Bunge la Jimbo la Illinos (Illinois Senate) tangu 1997 hadi 2004. Baada ya kushindwa katika jitihada zake za kuchaguliwa katika Bunge Dogo la Marekani mwaka 2000, Obama alisimama kuchaguliwa katika Bunge la Maseneta la Marekani Novemba 2004.

 

Alitangaza kusimama kuchaguliwa kama Rais wa Marekani Februari 2007. Baada ya kampeni kali katika uteuzi wa Chama cha Democratic dhidi ya Hillary Clinton, aliteuliwa urais kwa tiketi ya chama hicho.

 

Katika uchaguzi wa urais wa Marekani wa mwaka 2008, alimshinda John McCain aliyekuwa ameteuliwa na Chama cha Republican, na akaapishwa kuwa Rais Januari 20, 2009. Oktoba 9, 2009 Obama alituzwa Tuzo ya Nobel ya Amani.

 

Utoto na Ujana

Baba yake Obama, mzee Husein Obama alikuwa Raia Marekani mwenye asili ya Kenya na alifariki dunia 1982. Mzee Obama alitoka Mkoa wa Nyanza nchini Kenya.   Mama yake, Ann Dunham, alikuwa raia wa Marekani  (Mzungu) kutoka Jimbo la Kansas. Alifariki mwaka 1995.

 

Wazazi hao wa Obama walifunga ndoa wakati ndoa kati ya watu weupe na weusi ilikuwa marufuku katika sehemu za kusini mwa Marekani. Wazazi waliachana baada ya miaka miwili na mtoto Barack alibaki na mama Baadaye mama yake aliolewa na mwanafunzi kutoka Indonesia na akamfuata aliporudi kwake. Hivyo Barack aliishi Jakarta hadi 1971 aliporudi Marekani na kukaa na babu yake huko Hawaii hadi alipomaliza shule ya sekondari. Barack ana dada mmoja kutoka ndoa ya pili ya mama yake na baba wa kambo kutoka Jakarta, Indonesia.

 

Masomo na Kazi

Baada ya kumaliza masomo ya sekondari, alisomea masuala ya siasa na sheria katika vyuo vya Occidental huko Los Angeles, Columbia huko New York na baadaye Chuo Kikuu cha Harvard 1991 alipomaliza kwa shahada ya dokta.

 

Baada ya shahada ya kwanza, Obama alifanya kazi ya kijamii huko Chicago. Mwaka 1991 alirudi Chicago alipopata kazi katika Ofisi ya Mwanasheria akafundisha pia kozi za sheria kwenye Chuo Kikuu cha Chicago.

 

Akizungumza baada ya kubainika wazi kuwa ameshinda tiketi ya chama chake, Obama alisema, “Wakati maalum kwa taifa letu. Ninaikabili changamoto hii kwa unyenyekevu mkubwa, na kikomo cha ufahamu wangu. Lakini pia ninaikabili kwa imani isiyo kikomo mbele ya wananchi wa Marekani.”

 

Kipenzi cha Vyombo vya Habari

Obama alishamiri katika siasa za kitaifa na kimataifa kwa mara ya kwanza – akitumia hotuba maridadi aliyotoa kwenye Mkutano Mkuu wa uchaguzi wa chama cha Democratic mwaka 2004.

 

Obama alisisitiza historia yake binafsi katika hotuba iliyoakisi uimara wa jamii ya jadi ya Marekani, kujitegemea na matumaini.

 

“Kutokana na kufanya shughuli zake kwa bidii na ustahamilivu, baba yangu alipata nafasi ya kuja kusoma nchini Marekani, ambayo ni nguzo ya uhuru na fursa kwa watu wengi waliokuja kabla,” alieleza.

 

Baada ya kupata ushindi mkubwa katika uchaguzi wa Seneti, miezi michache baadaye alikuwa kipenzi cha vyombo vya habari na mmojawapo wa wanasiasa wenye mvuto katika siasa za Washington, huku akiwa ameandika vitabu viwili vilivyopata mauzo makubwa.

 

Alipata kuungwa mkono na mwendesha kipindi cha televisheni maarufu Oprah Winfrey, ambaye mbali ya kumshawishi atangaze nia yake ya kugombea kupitia kipindi chake, pia alimsaidia kupiga kampeni.

 

Watu takriban 30,000 walihudhuria mkutano uliofanyika South Carolina mwaka 2007 ambapo Winfrey alimwelezea Obama kuwa mtu mwenye kusikiliza mawazo ya wengine na ualimu uliojikita katika kusema ukweli.

 

Seneta huyo pia amevunja rekodi zote za kuchangisha fedha za kampeni, akitumia mtandao (internet) kukusanyia michango midogo midogo, pamoja na michango mikubwa kutoka kampuni kubwa.

 

Akiwa Seneta wa Illinois, amechukua msimamo wa kati kwenye upigaji kura ndani ya Baraza la Seneti, lakini pia ameshirikiana na wanasiasa wa Republican kwa masuala kama elimu ya kujikinga na Ukimwi.

 

Makuzi ya kimataifa

Obama ana jina la baba yake, aliyezaliwa na kukulia Kenya na kuchunga mbuzi – alifika Marekani baada ya kupata nafasi ya kusoma Hawaii.  Ingawa baba yake mzazi na baba yake wa kambo walikuwa Waislamu, Barack Obama ni Mkristo na alihudhuria shule za kawaida pia ya Kikatoliki kwa kipindi cha miaka minne aliyoishi Indonesia, nchi yenye idadi kubwa ya Waislamu.

 

Rangi

Seneta huyo alikuwa muumini wa Trinity United Church of Christ huko Chicago, kanisa moja huko Chicago, kwa takriban miongo miwili, lakini alijitoa Mei 2008 baada ya kugundulika mahubiri yenye utata kwa wachungaji wa Kanisa la Trinity.

 

Mchungaji Jeremiah Wright alinukuliwa akisema mashambulio ya Septemba 11, 2001 yalikuwa adhabu kwa Marekani kutokana na kuona watu weusi kuwa “nusu binadamu”. Akikusudia kutuliza mtafaruku huo, Obama alikabiliana na suala la rangi akitoa wito kwa Marekani kupiga hatua ya kurekebisha ukosefu wa haki katika misingi ya rangi.

 

Obama alipinga vita ya Iraq tangu mwanzo, alikuwa akizungumza wazi wazi kukosoa mipango ya kuivamia nchi hiyo miezi kadhaa kabla ya Machi 2003.

 

Mtizamo wake wa kujadiliana na viongozi wa Iran bila masharti umekosolewa na mpinzani wake wa Republican katika uchaguzi wa rais. Obama mara kwa mara amekuwa akitania kwamba watu wanakosa kutaja jina lake, wengine wakimwita “Alabama” au “Yo Mama”.

 

Hata nyota yake ikizidi kung’ara na umaarufu kuongezeka katika harakati za kampeni za uchaguzi, inaonekana kuwa bado kuna baadhi ya watu wanaolikosea jina lake.

 

Michelle Obama

Michelle LaVaughn Obama alizaliwa Januari 17, 1964. Kitaaluma ni Mwanasheria wa Marekani. Michelle alikulia katika kitongoji cha kusini mwa Chicago, na kusoma hadi Chuo Kikuu cha Princeton, baadaye katika Kitivo cha Sheria cha Harvard.

 

Baada ya kumaliza elimu yake hiyo, alirudi Chicago na kufanya kazi katika Kampuni ya Sidley Austin, na baadaye kuwa kama mmoja kati ya wafanyakazi wa Meya wa Chicago, Richard M. Daley. Pia alifanya kazi katika Chuo Kikuu cha Chicago na Hospitali za Chuo Kikuu cha Chicago.

 

Michelle Obama ni dada wa Craig Robinson, kocha wa mpira wa Kikapu wa Oregon State University. Alikutana na Barack alipojiunga na Sidley Austin.