BAVICHA WASHANGAA LOWASSA KUMPONGEZA MAGUFULI

BARAZA la Vijana la Chama cha Demokrasia na Maendeleo – Chadema (Bavicha) limesema limeshtushwa na Mjumbe wa Kamati Kuu ya chama hicho, Edward Lowassa, kumpongeza Rais John Magufuli kwa yale anayoyafanya.

Akizungumza leo Alhamisi Januari 11, Katibu wa Bavicha, Julius Mwita amehoji kuwa Lowassa amepata wapi ujasiri wa kumpongeza Rais huku akidai nchi inakabiliwa na matukio mengi ya uvunjaji wa haki za binadamu.

 

“Unampongezaje Rais Magufuli wakati serikali yake bado haijatoa tamko lolote tangu Mwanasheria wa Chadema, Tundu Lissu apigwe risasi Dodoma? Wakati huohuo serikali yake imezuia mikutano ya vyama vya siasa,” alisema Mwita.

Aidha, Mwita amesema kitendo cha Lowassa kumpongeza Rais Magufuli kimewasikitisha hasa kutokana na mazingira ya kisiasa yalivyo hapa nchini.

“Vyama vyetu vya upinzani vina malalamiko mengi wala hatukutegemea kiongozi wetu kusimama na kumpongeza mtu anayevikwamisha vyama vya siasa,” alisema Mwita.